• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
Gor Mahia wasajili fowadi matata Fonseca kutoka Brazil

Gor Mahia wasajili fowadi matata Fonseca kutoka Brazil

Na CHRIS ADUNGO

MABINGWA mara 19 wa Ligi Kuu ya Kenya, Gor Mahia, wamemsajili fowadi raia wa Brazil, Wilson Fonseca kutoka kambini mwa Fortaleza FC nchini Brazil.

Nyota huyo alitambulishwa rasmi kwa mashabiki mnamo Janauri 29 kupitia video ya Youtube iliyokuwa ikimwonyesha Fonseca akipokelewa na kocha Vaz Pinto na baadhi ya wachezaji na maafisa wa mazoezi wa Gor Mahia uwanjani Camp Toyoyo, Nairobi.

Huenda Fonseca akawajibishwa kwa mara ya kwanza na Gor Mahia katika mchuano wa FKFPL utakaowamutanisha na Bandari FC mnamo Januari 31, 2021 uwanjani Mbaraki Sports Complex, Mombasa.

“Kikosi cha Gor Mahia kitahitaji angalau wiki sita hivi ili kuzoea mbinu zangu za ukufunzi. Nimesimamia mechi nne pekee na nilipotwaa mikoba ya mabingwa hawa, kikosi kilikuwa na mrundiko wa mechi. Hivyo, hatukuwa na muda wa kutosha kujiandaa vilivyo kwa baadhi ya michuano,” akasema Pinto.

Tangu Pinto apokezwe mikoba ya Gor Mahia, klabu hiyo imecheza jumla ya mechi sita chini ya kipindi cha siku 18.

“Mrundiko wa mechi ni kiini cha kuchoka kwa wanasoka ambao wamekuwa wakisakata mchuano kila baada ya siku tatu,” akaongeza kwa kusisitiza kwamba kubwa zaidi katika maazimio yao baada ya kupepetana na Bandari FC, ni kujiandaa vilivyo kwa gozi la Mashemeji litakalowakutanisha na AFC Leopards mnamo Februari 10.

  • Tags

You can share this post!

Ibrahimovic na Lukaku wapigwa marufuku ya mechi moja kila...

Chelangat atetea taji la Mbio za Nyika za Kenya Police bila...