• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Gor yarejea kileleni baada ya Tusker kulewa magoli ya Wazito

Gor yarejea kileleni baada ya Tusker kulewa magoli ya Wazito

Na CECIL ODONGO

GOR Mahia jana waling’oa Tusker juu ya jedwali la Ligi Kuu ya Kenya (KPL) baada ya kuwapiga Ulinzi Stars mabao 2-0 huku Wanamvinyo hao wakitandikwa 2-1 na Wazito katika Kaunti ya Kisumu.

K’Ogalo ilivuna ushindi huo muhimu katika uwanja wa Kasarani huku Tusker nao wakipigwa na Wazito kwenye uwanja ‘hatari’ wa Muhoroni.

Gor sasa wanaongoza KPL kwa alama 67kutokana na mechi 32, huku Tusker ikikamata nafasi ya pili kwa alama 65.

Kutokana na ushindi dhidi Tusker, Wazito waliimarisha nafasi yao ya kutoshushwa ngazi msimu huu.

Wazito sasa wana alama nne mbele ya Mathare United ambao walipoteza 1-0 dhidi ya Kakamega Homeboyz katika uwanja wa Bukhungu, Kakamega.

Wazito na Mathare watachuana katika mechi ya mwisho ya KPL hapo Juni 24 huku timu hizo mbili zikikodolewa na hatari ya kutemwa katika ligi kuu.

Timu ambayo itakamilisha KPL katika nafasi ya 16 itachuana na ile ambayo itamaliza nambari tatu kwenye Ligi ya Taifa (NSL) kisha mshindi ashiriki ligi kuu ya KPL msimu ujao.

Kwenye mechi nyingine ambazo ziliandaliwa jana, Vihiga Bullets ambao tayari wameshushwa ngazi walishangaza AFC Leopards kwa kuwapiga 2-1 katika uga wa Mumias Complex, Kakamega.

Kenya Police nao walishinda Posta Rangers 3-1 kwenye uga wa Police Sacco.

KCB ambao hawasaki ubingwa tena, walishinda Bidco United 1-0 katika uga wa Kasarani Annex.

Kuelekea mechi ya jana, Tusker walikuwa mbele ya Gor kwa alama moja ila sasa K’Ogalo wako pazuri kutwaa ubingwa wa KPL iwapo watashinda mechi zao mbili zilizosalia.

Mabao ya Gor yalifungwa na Austin Odhiambo na John Macharia dakika 10 za mwanzo na kuwapa ushindi huo muhimu.

  • Tags

You can share this post!

Bado nasubiri jibu la demu miaka 2 sasa!

Waititu amezirai nyumbani, wakili aambia korti katika kesi...

T L