• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
Homeboyz wakiri ni pigo kwao kupoteza wanaraga wanne

Homeboyz wakiri ni pigo kwao kupoteza wanaraga wanne

AYUMBA AYODI na GEOFFREY ANENE

Klabu ya raga ya Homeboyz huenda imetikiswa na kuondoka kwa wachezaji wanne na kukosa kurejea kwa kocha, lakini hawajakufa matumaini wanapojiandaa kwa msimu mpya.

‘Madeejay’ hao wamepoteza washambuliaji tegemeo Joshua Chisanga, Emmanuel Mavala na Philip Ikambili na mpigaji wa kiki Evin Asena, ambao wote wamejiunga na Kenya Harlequin.

Kuharibu mambo zaidi kocha wao kutoka Afrika Kusini Jason Hector hajarejea nchini tangu Kenya itangaze kufunga mipaka yake mwezi Machi 2020 kuzuia maambukizi ya virusi vya corona. Tetesi zinasema Hector amepata kazi nchini mwake.

Mwenyekiti wa Homeboyz Mike Rabar na kocha Simon Odongo wanaamini kuwa wachezaji waliobaki wana uwezo wa kujituma kiasi cha kuzua ushindani.

“Tuna kundi la wachezaji karibu 200 na nadhani pia hii ni fursa ya chipukizi kujionyesha,” alisema Rabar na kuongeza kuwa Homeboyz ilicheza mechi sita za mwisho za msimu 2019-2020 bila nyota hao ambao wamehamia Quins.

Homeboyz ilikamilisha msimu wa kawaida katika nafasi ya tatu kwa alama 66 kabla ya mkurupuko wa virusi vya corona kusababisha awamu ya muondoano kusimamishwa kwa ghafla. Mshindi hakupatikana msimu huo kwa sababu mechi za muondoano zilifutiliwa mbali.

Msimu mpya wa Ligi Kuu ya Kenya Cup unafaa kuanza Februari 27, lakini Rabar alitilia shaka tarehe hiyo akisema serikali bado haijaidhinisha mazoezi ya kugusana yaanze.

“Timu nyingi zinaendesha mazoezi ya wachezaji kufanya mazoezi kivyao ambayo yanajumuisha mazoezi ya viungo vya mwili na yale yanayofanywa kwenye chumba cha mazoezi,” alisema Rabar akidokeza kuwa bado wanahitaji huduma za Hector.

“Bila shaka, tumetikiswa hasa baada ya kupoteza wachezaji hao muhimu. Itaturudisha hatua kadhaa nyuma, lakini tutainuka tukiwa na nguvu zaidi,” alisema Odongo na kuongeza kuwa changamoto itakuwa jinsi wachezaji waliobaki wataongeza juhudi zao.

Odongo alisema kuwa mikakati iliyofanywa na Hector bado ina nguvu na itaendelea kutumika. “Tunafaa kuendelea na mahali tulipoacha msimu uliopita bila tatizo. Tutalenga kudhibiti chombo chetu jinsi ilivyokuwa msimu uliopita na kufika nusu-fainali.”

Homeboyz wamesajili mchezaji mmoja pekee ambaye ni Ochieng kutoka Nondescripts, lakini Odongo ametupia jicho kupandisha daraja wachezaji kutoka timu ya Homeboyz inayoshiriki kipute cha Eric Shirley Shield.

Chipukizi hao ni wachezaji wa timu ya taifa ya Under-20 Arnold Onyere na Ronald Ngaira na winga Pius Odera kutoka Shule ya Upili ya Upper Hill.

Odongo alikiri Homeboyz imekuwa ikipitia changamoto ya wachezaji kadhaa kukosekana kwa sababu si wachezaji wote wamerejelea mazoezi. “Wachezaji wengine waliamua kujiingiza katika shughuli nyingine wakati michezo ilipigwa marufuku. Huwezi kuwaita warejee bila mpango, hasa kwa sababu hakuna mwelekeo mzuri kuhusu masharti ya kudhibiti virusi vya corona,” alisema Odongo akiongeza kuwa fedha zitakiwa mzigo Mkubwa.

You can share this post!

Jaji aliyemzima Mwilu amrudisha kuwa Kaimu Jaji Mkuu

‘Simba’ wa Kisii kukumbukwa kwa kunguruma