Na PATRICK KILAVUKA
Kocha wa Kangemi Athletico Geofrey Muganda alisema ushindi wa 3-1 dhidi ya RYSA Academy katika Ligi ya Kaunti, FKF, Nairobi West,Jumapili uwanjani Kihumbuini, ulitokana na mchezo safi wa uwiano na kujipanga vyema uwanjani mbali na kutumia nafasi zao vyema.
Magoli ya Athletico yalipachikwa na Charles Otenya(mawili) dakika ya 17 na 29 na Levin Manoa dakika ya 44 ilhali Academy walifuta machozi dakika 28 kupitia David Lumumba.
Katika mchuano mwingine, Kangemi PAG walizoa ushindi wa 2-1 mbele ya Hillside, Ngong. Moses Wanyama ndiye alikuwa mtia fora katika patashika hilo alipofunga mawili dakika ya nne na 28 kabla Kevin Otieno kujibu la pekee la Hillside kunako dakika ya 76.
Kwingineko, Silver Bullets walifyatua Missisippi FC makombora 3-1 na kujiongezea matumaini ya kufamya vyema katika ligi ya FKF, kaunti ndogo ya Kabete, wadi ya Lower Kabete, uwanjani Approved, wikendi.
Wafyatuaji walikuwa James Chaloba kunako dakika ya 46,Nicholas Mwangi dakika ya 59 na Ben Andira dakika ya 88. Hata hivyo, Missisippi ndio walikuwa wa kwanza kucheka na nyavu kupitia Carbini Maina dakika ya 13.
Katika mechi nyingine, Wangige Hotstars walizima Kabete Pirates 2-0 kupitia magoli yote ya Newton Njoroge dakika ya kwanza na 77.