Na JOHN KIMWERE
MCHEZAJI wa kimataifa, Erick Kapaito inaonekana ameanza kufufua kasi yake kwenye kampeni za Ligi Kuu nchini Ethiopia baada ya kufungia klabu yake Arba Minch City mabao manne ndani ya wiki moja.
Mnamo Jumapili mchezaji huyo aliyejiunga na klabu hiyo akitokea Kariobangi Sharks ya Kenya alitikisa nyavu mara mbili na kusaidia klabu yake kusajili ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Dire Dawa City.
Ufanisi huo ulikuwa baada ya kucheka na nyavu mara mbili na kubeba kikosi hicho kutwaa ushindi wa mabao 2-1 mbele ya Sidama Coffee Jumanne iiliyopita.
Mchezaji huyo ameanza kutesa licha ya kuanza kampeni zake kwa kasi ya chini katika kipindi cha uhamisho.
Kwenye patashika ya Jumapili, ilichukua Arba Minch City dakika 14 kupata bao la kwanza kupitia penalti iliyochanjwa na Bernard Ochieng.
Kapaito alifunga mabao hayo kupitia penalti. Mwanzo wapinzani wao walipata adhabu baada ya Daniel Damisse kuangusha eneo hatari pale Kapaito alipoiga mkwaju uliochangia mlindalango kuruka bila kuuona mpira.
Kapaito alitikisa nyavu kwa mara ya pili alipopiga penalti baada ya yeye mwenyewe kuangushwa ndani ya kijisaduku na Mesay Paulos Dana dakika ya 77.