Na GEOFFREY ANENE
DEREVA McRae Kimathi ameelekea nchini Ureno kushiriki duru ya nne ya Mbio za Magari Duniani (WRC) itakayofanyika Mei 19-22.
Bingwa huyo wa Afrika wa kitengo cha chipukizi alikuwa Uganda wikendi iliyopita (Mei 6-8) kwa duru ya Afrika ya Pearl ambapo alimaliza nambari tisa kwa jumla, nambari nne katika kitengo cha washiriki wa duru za Afrika na nambari moja katika kitengo cha chipukizi. Alishirikiana na mwelekezi wake Mwangi Kioni katika gari la Ford Fiesta R3.
Katika kampeni za Afrika (ARC), Kimathi anapatikana katika nafasi ya tano kwa alama 28. Nafasi nne za kwanza zinashikiliwa na Mzambia Leroy Gomes (78), Mkenya Karan Patel (45), Giancarlo Davite kutoka Rwanda (30) na Mganda Jas Mangat (30).
Kimathi alishiriki duru za dunia za Uswidi (Februari 24-27) na Croatia (Aprili 21-24). Baada ya Ureno, Kimathi atashiriki duru nyingine za dunia za Estonia (Julai 14-17), Safari Rally (Juni 23-26) na Ugiriki (Septemba 8-11).
Anashikilia nafasi ya saba (mwisho) katika msimamo wa pointi za Mbio za Magari Duniani za chipukizi (JWRC) kwa alama 12. Alikamata nafasi ya nne nchini Uswidi na kukosa kukamilisha nchini Croatia.