• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 2:24 PM
Kocha Beldine Odemba ataja wachezaji 30 wa kuwinda tiketi ya WAFCON

Kocha Beldine Odemba ataja wachezaji 30 wa kuwinda tiketi ya WAFCON

NA TOTO AREGE

KOCHA mpya wa timu ya taifa ya Harambee Starlets, Beldine Odemba mnamo Jumanne ametaja kikosi cha wachezaji 30 kwa maandalizi ya mechi za mchujo wa kufuzu kwa Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2024.

Kenya itamenyana na Indomitable Lionesses ya Cameroon mnamo Septemba 22, 2023 katika mkondo wa kwanza ikifuatiwa na mkondo wa pili nyumbani mnamo Septemba 26, 2023.

Hii itakuwa mechi ya kwanza ya kimataifa kwa Starlets tangu Kenya kuanza tena soka ya kimataifa baada ya marufuku iliyokuwa imewekewa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

Marufuku hayo yaliondolewa mnamo Novemba 2022.

Odemba alichukua usukani wiki moja iliyopita kutoka kwa kocha Godfrey Oduor ambaye alijiuzulu.

Amefanya mabadiliko katika kikosi, tofauti na kile kilichotajwa na Oduor kumenyana na Albania katika mechi ya kirafiki mapema mwaka huu wa 2023.

Amemjumuisha mshambulizi matata Valerie Nekesa kutoka Soccer Assassins na beki Quinter Owiti kutoka Kenya Police Bullets FC. Wawili hao, walivutia wakiwa timu na kikosi cha Rising Starlets

Nekesa alifanya vyema katika Ligi ya Daraja la Kwanza 2022/23 ambapo, alishinda Kiatu cha Dhahabu kwa kufunga mabao 37 katika mechi 22.

Wachezaji wengine wageni ni Airin Madalina, mshindi wa Kiatu cha Dhahabu cha msimu wa 2022/23 Ligi Kuu ya Wanawake ya Shirikisho la Soka nchini (FKF-WPL) kutoka Bunyore Starlets na kipa Caroline Rufa wa Simba Queens ya Tanzania.

Mchumani watakuwepo wazoefu Valentine Khwaka, Diana Tembesi na Annedy Kundu.

Mabeki Enez Mango, Wincate Kaari, Ruth Ingosi na Vivian Nasaka wameaminiwa katika majukumu ya ulinzi.

Winga Mercy Airo ameitwa baada ya kuwa nje kwa muda mrefu. Washambuliaji wengine mashuhuri, Marjolene Nekesa na Esse Akida wamejumuishwa kwenye kikosi hicho.

Wachezaji wa kati watadhibitiwa na Cynthia Shilwatso, Sheryl Angachi, Ketsia Ngaira, Vivian Corazone, Marjolene Nekesa na Mercyline Anyango.

Jentrix Shikangwa Topista Situma, Elizabeth Wambui na Mwanalima Adam wataongoza safu mashambulizi

Timu itaripoti kambini Jumapili, Septemba 10, 2023, kuanza maandalizi ya raundi hiyo muhimu ya kufuzu.

Mshindi kati ya Kenya na Cameroon baadaye atachuana na mshindi kati ya Gabon na Botswana kati ya Novemba 27 na Desemba 5, 2023, ili kukata tiketi ya shindano hilo litakaloandaliwa Morocco mwaka 2024.

Kikosi cha muda

Makipa: Valentine Khwaka (Kenya Police Bullets FC), Annedy Kundu (Ness Atromitou FC) na Caroline Rufa (Simba Queens)

Mabeki: Christine Awuor (Zetech Sparks), Lavender Atieno Okeyo (Kenya Police Bullets FC), Phoebe Owiti (Vihiga Queens), Dorcas Shikobe (Sirines of Grevena), Enez Mango (Farul Constanta), Wincate Kaari (Yanga Princess), Ruth Ingosi (Simba Queens), Vivian Nasaka (Hakkarigucuspor), Quinter Owiti (Kenya Police Bullets FC)

Viungo wa Kati: Cynthia Shilwatso (FC Kryvbas Women), Sheryl Angachi (Ulinzi Starlets), Ketsia Ngaira (Ulinzi Starlets), Vivian Corazone (Simba Queens),  Marjolene Nekesa(SK Slavia Praha), Mercyline Anyango (JFK Panthers)

Washambulizi: Jentrix Shikangwa (Beijing Jingtan FC), Topista Situma (Fountain Gates Princess), Elizabeth Wambui (Simba Queens), Mwanalima Adam (Hakkarigucuspor), Airin Madalina (Bunyore Starlets), Esse Akida (FC PAOK), Tereza Engesha (Hyundai Steel R.A), Purity Alukwe (Kenya Police Bullets FC), Violet Nanjala (AMLFF LAAYOUNE), Valerie Leah Nekesa (Soccer Assassins), Mercy Airo (Ulinzi Starlets) na Janet Moraa Bundi (Vihiga Queens).

  • Tags

You can share this post!

Salasya akwepa swali kuhusu mabadiliko ya tabianchi

Kioja Gachagua akimsalimu Raila baada ya kuapa awali...

T L