Na MASHIRIKA
KOCHA Frank Lampard amesema haogopi kabisa kupigwa kalamu ugani Goodison Park licha ya msururu wa matokeo duni yaliyoshuhudia kikosi chake cha Everton kikipepetwa na West Ham United 2-0 ugani London Stadium, Jumamosi.
Everton almaarufu Toffees, hawajashinda mechi yoyote ya EPL tangu Oktoba 2022 na sasa wanakamata nafasi ya 19 jedwalini kwa alama 15 sawa na Southampton wanaovuta mkia.
Fomu mbovu ya Everton ambao wamepoteza mechi sita na kupiga sare mbili kutokana na michuano minane iliyopita, imeshuhudia Lampard akikamilisha kipindi kirefu zaidi bila ushindi katika historia yake ya ukufunzi ligini.
Lampard amevunia waajiri wake alama moja pekee kutokana na mechi tisa zilizopita za EPL – dhidi ya Man-City (1-1) – na ameshindia kikosi hicho mechi tatu pekee kati ya 20 hadi sasa muhula huu.
“Sina hofu ya kutimuliwa kwa sababu nafanya kazi yangu. Naamka kila asubuhi nikiwa la lengo la kukwamua kikosi ila bahati haijakuwa ikisimama,” akasema Lampard.
Mechi dhidi ya Palace ilikuwa ya kwanza kwa mmiliki wa Everton, Farhad Moshiri, kuhudhuria katika kipindi cha miezi 14. Bwanyenye huyo alipoulizwa iwapo ana mpango wa kumfurusha Lampard, alisema: “Sina maoni. Hayo si maamuzi yangu.”
Kushuka kwa makali ya Everton kumewashuhudia pia wakidenguliwa kwenye raundi ya tatu ya vipute vya Carabao Cup na Kombe la FA msimu huu.
MATOKEO YA EPL (Jumamosi):
Liverpool 0-0 Chelsea
Bournemouth 1-1 Forest
Leicester 2-2 Brighton
Southampton 0-1 Aston Villa
West Ham 2-0 Everton
Palace 0-0 Newcastle
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO