• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 4:40 PM
Kocha Koeman atoa orodha ya wachezaji sita anaotaka Barcelona wasajili mwishoni mwa msimu huu

Kocha Koeman atoa orodha ya wachezaji sita anaotaka Barcelona wasajili mwishoni mwa msimu huu

Na MASHIRIKA

BARCELONA wamefichua orodha ya wanasoka sita ambao kocha Ronald Koeman amewapendekezea kusajili mwishoni mwa msimu huu.

Huku rais mpya wa kikosi hicho, Joan Laporta akiwa mwingi wa matumaini kwamba kigogo Lionel Messi atarefusha mkataba wake ugani Camp Nou, kinara huyo amekiri kwamba wanahitaji kujisuka upya kwa ajili ya misimu ijayo.

Kwa mujibu wa gazeti la Sport nchini Uhispania, fowadi Erling Braut Haaland ni miongoni mwa wanasoka wanaoviziwa na Barcelona ambao tayari wamekutana na baba wa nyota huyo raia wa Norway, Alf-Inge pamoja na wakala wake, Mino Raiola.

Haaland, 20, amefungia waajiri wake Borussia Dortmund jumla ya mabao 25 kutokana na mechi 26 Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) msimu huu na anahusishwa pakubwa na Manchester City na Real Madrid.

Kulingana na gazeti la Mundo Deportivo, Barcelona wako pazuri zaidi kujinasia maarifa ya Haaland ambaye amekuwa na matamanio ya kucheza pamoja na Messi tangu utotoni.

Iwapo Barcelona watashindwa kujinasia huduma za Haaland, basi watashawikisha zaidi kumsajili Sergio Aguero, 32, ambaye pia anawaniwa na Everton, Juventus na Napoli.

Koeman, 58, anamezea pia maarifa ya fowadi wa zamani wa Manchester United, Memphis Depay, aliyewahi kuwa chini ya uelekezi wake katika timu ya taifa ya Uholanzi. Sawa na Aguero, mkatabwa wa sasa wa Depay na Olympique Lyon ya Ufaransa unatamatika rasmi mwishoni mwa msimu huu.

Depay, 27, amefungia Lyon jumla ya mabao 19 na kuchangia mengine 10 kutokana na mechi 35 zilizopita za Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1).

Sogora mwingine anayehemewa na Barcelona ni fowadi Lautaro Martinez ambaye kwa pamoja na Romelu Lukaku, amekuwa tegemeo kubwa kambini mwa Inter Milan ambao ni mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Italia (Serie A). Haja ya kuendelea kushirikiana na Messi katika ngazi ya klabu sawa na jinsi ilivyo katika kiwango cha timu ya taifa huenda ikamchochea Martinez kuyoyomea Barcelona.

Fowadi huyo mwenye umri wa miaka 23 amefungia Inter jumla ya mabao 15 na kuchangia mengine manane kwenye kampeni za Serie A muhula huu.

Sogora mwingine ambaye anahusishwa pakubwa na Barcelona ni kiungo matata wa Liverpool, Georginio Wijnaldum na beki Eric Garcia wa Man-City.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Trump azindua blogu ya kuchapisha taarifa muhimu kutoka...

Man-United tayari kuweka mezani Sh13 bilioni kwa ajili ya...