• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
Kocha Wayne Rooney ataka vinara wa Derby County wamwachishe kazi haraka iwezekanavyo

Kocha Wayne Rooney ataka vinara wa Derby County wamwachishe kazi haraka iwezekanavyo

Na MASHIRIKA

WAYNE Rooney ametaka wasimamizi wa klabu ya Derby County “kumwachisha kazi ya ukocha mara moja.”

Rooney, 36, angali na mwaka mmoja katika kandarasi yake ya sasa na kikosi cha Derby County ambacho kiliteremshwa ngazi hadi Ligi ya Daraja ya Pili nchini Uingereza (League One) mwishoni mwa msimu wa 2021-22.

“Nahisi kwamba kikosi hiki kwa sasa kinastahili kunolewa na mtu mwingine atakayeleta nguvu mpya, mtu ambaye hakuathiriwa na matukio ambayo yameshuhudiwa kikosini kwa miezi 18 iliyopita,” akasema Rooney.

Rooney ambaye ni mchezaji wa zamani wa Everton, Manchester United na timu ya taifa ya Uingereza, amesema amekuwa akifuatilia kwa karibu matukio ya hivi karibuni katika kikosi cha Derby County kinachotarajiwa kutwaliwa na wamiliki wapya.

Umiliki wa kikosi cha Derby County unatarajiwa kutwaliwa na bwanyenye David Clowes ambaye tayari amenunua uwanja wa Pride Park stadium.

Rooney ndiye anashikilia rekodi ya mfungaji bora wa muda wote kambini mwa Uingereza kwa mabao 53 kutokana na mechi 120 za kimataifa. Alijiunga na Derby County mnamo Januari 2020 akiwa mchezaji baada ya kuvalia jezi za DC United ya Amerika katika Major League Soccer (MLS).

Aliaminiwa kushikilia mikoba ya ukufunzi kambini mwa kikosi hicho mnamo Novemba 2020 na akaajiriwa kwa mkataba wa miaka miweili na nusu miezi mitatu baadaye.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Liverpool na Salah wavutania mshahara

Mpasuko Azimio kuhusu ‘mchujo’

T L