• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 7:55 AM
Leeds wazima Chelsea katika EPL uwanjani Elland Road

Leeds wazima Chelsea katika EPL uwanjani Elland Road

Na MASHIRIKA

LEEDS United waliendeleza mwanzo bora wa kutoshindwa katika mechi tatu za ufunguzi wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) muhula huu kwa kupepeta Chelsea 3-0 mnamo Jumapili ugani Elland Road.

Licha ya kutumia zaidi ya Sh24 bilioni kujisuka upya muhula huu, Chelsea walizidiwa maarifa na Leeds katika kila idara na wakafungwa mabao mawili kufikia mwisho wa kipindi cha kwanza.

Masihara ya kipa Edouard Mendy yalimpa fowadi Brenden Aaronson fursa nzuri ya kuwaweka Leeds uongozini katika dakika ya 33, sekunde chache kabla ya Rodrigo kushirikiana na Jack Harrison na kujaza kimiani goli lake la nne msimu huu.

Kutokuwepo kwa N’Golo Kante anayeuguza jeraha katika kikosi cha kwanza cha Chelsea, kuliwapa Leeds fursa ya kutamalaki mchezo katika safu ya kati na kuzuia vilivyo mashambulizi yote ya masogora wa kocha Thomas Tuchel.

Ilikuwa mara ya kwanza kwa Leeds kuangusha Chelsea ligini baada ya kutofaulu katika majaribio saba ya awali tangu mwaka wa 2002.

Chelsea walikamilisha mchuano huo wakiwa na wachezaji 10 pekee uwanjani baada ya sajili wao mpya, Kalidou Koulibaly, kuonyeshwa kadi nyekundu mwishoni mwa kipindi cha pili.

MATOKEO YA EPL (Jumapili):

Leeds 3-0 Chelsea

West Ham 0-2 Brighton

Newcastle 3-3 Man-City

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Beki Ouma afungia AIK bao tamu ikilipua Norrkoping

Chaguzi zilizoahirishwa Mombasa, Kakamega sasa kufanyika...

T L