• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 3:09 PM
Leopards, Sharks zapaa ligini huku Sofapaka na wanajeshi wa Ulinzi Stars wakiridhika na sare

Leopards, Sharks zapaa ligini huku Sofapaka na wanajeshi wa Ulinzi Stars wakiridhika na sare

Na CHRIS ADUNGO

AFC Leopards wamepaa hadi nafasi ya nne kwenye msimamo wa jedwali la Ligi Kuu ya Kenya baada ya kuwakung’uta Posta Rangers 2-1 uwanjani MISC Kasarani, Jumamosi.

Mabingwa hao mara 13 wa Ligi Kuu sasa wanajivunia alama 18 sawa na Kariobangi Sharks ambao pia walisajili ushindi wa 2-1 dhidi ya Nairobi City Stars.

Elvis Rupia aliwafungulia Ingwe ukurasa wa mabao katika dakika ya 30 kabla ya Bienvenue Shaka ambaye ni raia wa Tunisia kuongeza la pili dakika nne baadaye. Chini ya kocha Sammy ‘Pamzo’ Omollo, Rangers walifutiwa machozi na Calvin Odongo mwishoni mwa kipindi cha pili.

Baada ya Leopards kuwapiga Rangers sasa ni pengo la pointi mbili pekee ndilo linalowatenganisha Ingwe na Tusker wanaojivunia alama 20 sawa na Wazito FC waliowacharaza Kakamega Homeboyz 1-0 ugani Bukhungu, Kakamega.

Kwa upande wao, Rangers wanakamata nafasi ya 11 kwa alama 10 sawa na City Stars. Wakicheza dhidi ya City Stars, Sharks walikuwa wa kwanza kuliona lango la wenyeji wao kupitia bao la Julius Masaba katika dakika ya 13 kabla ya Davis Agesa kusawazisha mambo dakika 20 baadaye. Fowadi Eric Kapaito ndiye alifungia Sharks bao la ushindi dakika tisa kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mechi kupulizwa.

Huku Sharks wakijiweka sawa katika orodha ya wagombezi halisi wa taji la FKFPL muhula huu, City Stars walisalia katika nafasi ya 10 kwa alama 10 sawa na Rangers ambao pia wametandaza jumla ya michuano 10.

Mabingwa wa 2009, Sofapaka walikabwa koo na Vihiga United kwa sare ya 1-1 uwanjani Mumias Complex katika mechi nyingine ya Januari 30, 2021. Kepha Aswani aliwaweka Sofapaka kifua mbele katika dakika ya nne baada ya kukamilisha krosi ya kiungo Elli Asieche. Hata hivyo, Vihiga United walirejeshwa mchezoni na Patrick Okulo kunako dakika ya 39. Matokeo hayo yaliwasaza Batoto ba Mungu katika nafasi ya tisa kwa alama 11, mbili mbele ya Vihiga wanafunga orodha ya 12-bora.

Licha ya kulazimishiwa sare tasa na wanajeshi wa Ulinzi Stars uwanjani Afraha, Nakuru, wanabenki wa KCB wangali kileleni mwa jedwali kwa pointi 22, mbili zaidi kuliko Wazito FC na Tusker watakaowaalika Mathare United ugani MISC Kasarani mnamo Januari 31. Ulinzi Stars ambao ni mabingwa mara nne wa taji la Ligi Kuu wanashikilia nafasi ya sita kwa alama 13 sawa na Bandari FC watakaokuwa wenyeji wa Gor Mahia mnamo Januari 31 ugani Mbaraki Sports Complex, Mombasa.

MATOKEO YA FKFPL (Januari 30):

AFC Leopards 2-1 Posta Rangers

City Stars 1-2 Kariobangi Sharks

Ulinzi Stars 0-0 KCB

Vihiga United 1-1 Sofapaka

You can share this post!

Levante waduwaza Real Madrid kwa kuichapa 2-1 kwenye mechi...

Uhuru amsaga Ruto Sagana