• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 6:50 AM
Lewandowski afunga mabao matatu na kusaidia Barcelona kuponda Viktoria Plzen katika UEFA

Lewandowski afunga mabao matatu na kusaidia Barcelona kuponda Viktoria Plzen katika UEFA

Na MASHIRIKA

ROBERT Lewandowski alianza maandalizi ya kukutana na waajiri wake wa zamani, Bayern Munich, kwa kupachika wavuni mabao mabatu katika ushindi wa 5-1 uliosajiliwa na Barcelona dhidi ya Viktoria Plzen ya Jamhuri ya Czech katika mchuano wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Jumatano usiku ugani Camp Nou.

Lewandowski, 34, sasa ana mabao manane kutokana na mechi tano ambazo amesakatia Barcelona waliomsajili kutoka Bayern mnamo Julai 2022.

Gozi dhidi ya Viktoria lilikuwa la kwanza kwa nyota huyo raia wa Poland kufunga katika soka ya UEFA tangu aongoze Bayern kukomoa Paris Saint-Germain (PSG) na kunyanyua taji la kipute hicho mnamo 2019-20.

Magoli mengine ya Barcelona yalitiwa wavuni na Franck Kessie na Ferran Torres huku Viktoria wakifutiwa machozi na Jan Sykora.

Lewandowski ndiye mwanasoka wa kwanza katika historia kuwahi kufunga mabao matatu katika mchuano mmoja wa UEFA akivalia jezi za timu tofauti – Borussia Dortmund, Bayern Munich na Barcelona.

Kwa sasa anajivunia mabao 32 kutokana na mechi 20 zilizopita za UEFA katika hatua ya makundi.

Ushindi dhidi ya Viktoria unatarajiwa kuwapa Barcelona motisha zaidi kadri wanavyojiandaa sasa kuvaana na Bayern katika pambano la pili la Kundi C mnamo Septemba 13, 2022. Bayern walipepeta Inter Milan ya Italia 2-0 mnamo Jumatano usiku ugani San Siro.

Lewandowski alijiunga na Bayern bila ada yoyote mnamo 2014 baada ya kuagana na Dortmund. Alifungia Bayern mabao 50 kutokana na mechi 46 za msimu uliopita wa 2021-22 na kusaidia miamba hao kutwaa taji la 10 mfululizo la Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).

Anajivunia kufungia Bayern jumla ya mabao 344 kutokana na mechi 374 na ndiye wa pili nyuma ya Gerd Muller katika orodha ya wafungaji bora wa muda wote kambini mwa kikosi hicho.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Bayern Munich wapepeta Inter Milan katika pambano la UEFA...

Napoli yazamisha Liverpool na kuendeleza masaibu ya kocha...

T L