• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Limbukeni Shanderema walipuliwa na St Anthony’s

Limbukeni Shanderema walipuliwa na St Anthony’s

NA CECIL ODONGO

LIMBUKENI Shanderema waliokuwa wanawaka moto wamepigwa 1-0 na St Anthony’s Boys High School Kitale, ambao ni mabingwa mara tano wa michezo ya shule za upili, katika nusu fainali iliyogaragazwa uwanjani Bukhungu, Kaunti ya Bungoma.

Mshambuliaji mwenye ubunifu mkubwa, Aldrin Kibet amefunga bao hilo katika kipindi cha kwanza na kuihakikishia St Anthony fainali ya makala ya mwaka huu 2023.

Vijana wa kocha Peter Mayoyo wametandaza soka safi, mpira ukigusa nyasi huku wakigawana pasi safi kiasi kwa kuwashangaza mashabiki wa Shanderema ambao ndio walikuwa wengi uwanjani humo.

Hata Katibu Mkuu wa United Democratic Alliance (UDA) Cleophas Malala na aliyekuwa Mbunge wa Shinyalu Justus Kizito wamenyanyuka na kuwapigia makofi Solidarity Boys wa St Anthony pale walidhibiti mpira kwa dakika tano mfululizo.

Dakika 15 za mwisho, Shanderema wamekuwa na nguvu kuwazidi St Anthony lakini wakakosa kutumia fursa zao.

“Tulikuwa wazuri zaidi lakini katika kipindi cha pili Shanderema wametuonyesha kwamba nao wanajua kutandaza soka safi. Japo tumeshafuzu kushiriki mashindano ya Shule za Afrika Mashariki, la muhimu kwa sasa ni kubeba taji la kitaifa,” amesema kocha Mayoyo.

Baada ya mechi hiyo, mwanasiasa Malala amewatunuku St Anthony Sh300,000 nao Shanderema wakatuzwa Sh200,000.

  • Tags

You can share this post!

Katambe! Ngoma ya EPL yaanza rasmi leo Ijumaa

Mashabiki wa kandanda Lamu waipa Manchester City kichwa

T L