• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 10:50 AM
Limbukeni Sheriff Tiraspol washangaza Real Madrid kwa kichapo katika mechi ya UEFA ugani Bernabeu

Limbukeni Sheriff Tiraspol washangaza Real Madrid kwa kichapo katika mechi ya UEFA ugani Bernabeu

Na MASHIRIKA

SHERIFF Tiraspol waliduwaza Real Madrid ambao ni mabingwa mara 13 wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) kwa kichapo cha 2-1 katika mechi ya Kundi D mnamo Jumanne usiku uwanjani Santiago Bernabeu.

Sebastien Thill aliwafungia Sheriff bao la ushindi mwishoni mwa kipindi cha pili baada ya Karim Benzema kusawazishia Real kupitia penalti ya dakika ya 65. Jasurbek Yakhshiboev alikuwa amewaweka limbukeni Sheriff uongozini kunako dakika ya 25.

Licha ya kujivunia masupastaa wengine katika kikosi chao kilichopigiwa upatu wa kutamba katika uwanja wa nyumbani, Real walizidiwa maarifa katika takriban kila idara na wageni wao wanaoshiriki Ligi Kuu ya Moldova.

“Ni bao zuri na muhimu zaidi katika historia yangu kitaaluma. Tulicheza kwa kujiamini na bahati ikasimama nami nikafunga bao la ushindi dhidi ya miamba wa bara Ulaya,” akasema Thill aliyekuwa akivalia jezi za FC Tambov ya Urusi kwa mkopo mnamo 2020-21.

Japo Real walimiliki asilimia 76 ya mpira katika kipindi cha pili, walikosa kudhihirisha ukubwa wa uwezo wao huku makombora 11 pekee kati ya 31 yaliyoelekezwa langoni mwa Sheriff yakilenga shabaha.

“Nimesikitishwa sana na matokeo haya. Nadhani hii ni mechi tuliyostahili kushinda. Tulipoteza nafasi nyingi za wazi na kila kitu kikawaendea sawa wageni wetu,” akasema kocha Carlo Ancelotti.

Ingawa Sheriff bado ni limbukeni katika soka ya bara Ulaya, wanajivunia rekodi ya kushinda mataji 20 ya Ligi Kuu ya Moldova. Walishuka dimbani dhidi ya Real wakijivunia kufunga jumla ya mabao 11 nao wakifungwa goli moja kutokana na mechi mbili za Ligi Kuu.

Ushindi dhidi ya Real unamaanisha kwamba kikosi hicho sasa ni cha pili baada ya Arsenal mnamo 2005-06 kuwahi kushinda mchuano wa mkondo wa kwanza wa UEFA ugani Bernabeu.

Aidha, Sheriff ndiyo klabu ya pili baada ya Leicester City mnamo 2016-17 kuwahi kushinda mechi mbili za ufunguzi wa kampeni za UEFA katika hatua ya makundi wakiwa washiriki wa kivumbi hicho kwa mara ya kwanza.

Alama tatu kwa Real zingewawekea historia ya kushinda mechi 100 ya UEFA katika uwanja wao wa nyumbani wa Bernabeu.

  • Tags

You can share this post!

Luis Suarez awaokoa Atletico Madrid kinywani mwa AC Milan...

Liverpool waponda Porto bila huruma katika UEFA