• Nairobi
  • Last Updated May 7th, 2024 6:36 PM
Luis Suarez awaokoa Atletico Madrid kinywani mwa AC Milan kwenye gozi kali la UEFA

Luis Suarez awaokoa Atletico Madrid kinywani mwa AC Milan kwenye gozi kali la UEFA

Na MASHIRIKA

LUIS Suarez alifunga bao kupitia penalti mwishoni mwa kipindi cha pili na kusaidia waajiri wake Atletico Madrid kusajili ushindi wa 2-1 dhidi ya AC Milan katika gozi la Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Jumanne usiku ugani San Siro.

Atletico ya kocha Diego Simeone walipewa mkwaju wa penalti baada ya Pierre Kalulu wa Milan kunawa mpira ndani ya kijisanduku sekunde chache kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mchezo kupulizwa.

Wenyeji Milan walitandaza mchuano huo wakiwa na wanasoka 10 pekee uwanjani kwa takriban dakika 68 baada ya Franck Kessie kuonyeshwa kadi ya pili ya manjano kwa kucheza rafu.

Awali, Rafael Leao alikuwa amewapa Milan uongozi kunako dakika ya 20 kabla ya nyota Antoine Griezmann kusawazishia Atletico katika dakika ya 84.Ilikuwa mara ya pili kutokana na mechi tatu kwa Suarez kufungia Atletico bao la ushindi mwishoni mwa kipindi cha pili.

Nyota huyo raia wa Uruguay aliwahi kufunga mabao mawili ya dakika za mwisho katika ushindi wa 2-1 uliosajiliwa na Atletico dhidi ya Getafe mnamo Septemba 21, 2021.

Atletico kwa sasa wanashikilia nafasi ya pili kwenye Kundi B kwa alama nne, mbili nyuma ya viongozi Liverpool ambao hawajapoteza mechi yoyote. Porto wana alama moja huku Milan wakivuta mkia bila pointi yoyote.

AC Milan hawajashinda mechi yoyote kutokana na mechi sita mfululizo za soka ya bara Ulaya kwa mara ya kwanza huku mechi nne kati ya tano zilizopita kwa Atletico kutandaza katika mashindano yote zikishuhudia refa akichomoa kadi nyekundu.

  • Tags

You can share this post!

Club Bruges yaendeleza masaibu ya RB Leipzig kwenye UEFA

Limbukeni Sheriff Tiraspol washangaza Real Madrid kwa...