Na GEOFFREY ANENE
BEKI Mkenya Brian “Mandela” Onyango alionjeshwa dakika saba timu yake ya Mamelodi Sundowns ikifyeka TS Galaxy 1-0 kwenye Ligi Kuu ya Afrika Kusini, Jumapili.
Mabingwa watetezi Sundowns maarufu kama “Brazilians”, walizoa ushindi huo wa tatu mfululizo baada ya mshambuliaji Peter Shalulile kupachika bao hilo la pekee dakika ya 17 ugani Mbombela. Goli hilo ni la 11 la raia huyo wa Namibia.
Mandela aliingia uwanjani kama mchezaji wa akiba katika nafasi ya Andile Jali dakika ya 87, huku refa akiongeza dakika nne.
Kaizer Chiefs anayochezea kiungo Mkenya Anthony “Teddy” Akumu itaalika Swallows ugani FNB hapo Mei 12.
Sundowns inaongoza ligi hiyo ya klabu 16 kwa alama 57 baada ya kujibwaga uwanjani mara 26. Inafuatiwa na AmaZulu (50), Golden Arrows (43), Orlando Pirates (42) na Swallows (40) katika nafasi tano za kwanza. Pirates na Swallows zimesakata michuano 25. Chiefs inakamata nafasi ya tisa kwa alama 29 kutokana na mechi 26.