NA CECIL ODONGO
MABAO ya haraka katika kipindi cha pili jana Jumatano yaliisaidia Nzoia Sugar kuendelea kuongoza Ligi Kuu (KPL) baada kuichapa Kariobangi Sharks 3-1 ugani Utalii, Nairobi.
Mabingwa mara 19 wa KPL Gor Mahia nao waliduwaza Tusker 2-1 katika mechi kali uwanja wa MISC Kasarani.
Kiungo Sydney Ochieng aliiweka Gor mbele kipindi cha kwanza lakini Shami Kibwana akasawazishia Tusker kupitia mpira wa ikabu dakika ya 52.
Mshambuliaji Benson Omala alifunga bao lake la 12 kupitia mkwaju wa penalti dakika 84 na kuihakikishia Gor ushindi huo.
“Nimefurahi sana kwa sababu tumeshinda mechi ngumu. Kucheza dhidi ya Tusker ilikuwa ngumu hasa ikizingatiwa ni timu yenye bajeti kubwa. Tuliwakumbusha kuwa wanahitaji kusakata boli badala ya ‘kupura’ mpira tu,” akasema Kocha wa Gor Johnathan McKinstry.
Kocha wa Tusker Robert Matano naye alichemka kuwa Gor walizawidiwa mpira wa penalti akihisi timu yake haikutendewa haki.
“Leo (jana Jumatano) mliona kilichofanyika. Ile haikuwa penalti na ililazimishwa kwa sababu hata tukio lilikuwa nje ya penalti. Leo refa ndiye aliwapa Gor ushindi na siogopi kusema kuwa hatujapoteza kwa haki,” akasema Kocha wa Tusker Robert Matano.
Mkufunzi huyo aliitaka FKF ichukue hatua dhidi ya refa huyo ‘akimpongeza’ kwa kumpa Gor ushindi na kuionea timu yake.
KCB nayo iliilalaza Sofapaka 1-0 na kuendelea kuipa Gor na Nzoia shinikizo kileleni mwa jedwali.
Beki Maurice Odhiambo alifunga bao hilo kupitia mkwaju wa penalti dakika ya 17.Ugani Ruaraka, Mathare United ilipata ushindi wake wa pili msimu huu kwa kuilemea Bullets 1-0.
Mfumaji mahiri Daniel Otieno alicheka na nyavu za wapinzani dakika ya 86.Katika mechi nyingine iliyoanza mapema, Alvin Mang’eni alifunga mabao mawili kipindi cha pili na kuongoza Kenya Police kupata ushindi wa 2-1 dhidi ya Nairobi City Stars uga wa MISC Kasarani Annex.
Kwenye mechi ya Nzoia, Sharks walichukua uongozi kipindi cha kwanza kupitia Keith Imbali ila vijana hao wa kocha Salim Babu walirejea kipindi cha pili wakiwa na mori na kupata mabao matatu.
Magoli yao yalifumwa na John Mwangi, Felicen Okanda na Collins Obanda naye akajifunga dakika ya 73 na kutuku Nzoia ba la bure.
Nzoia sasa inaongoza ligi kwa alama 31 na huu ulikuwa ushindi wao wa tisa msimu huu.
Sharks nao wanaendelea kuuma huu baada ya kukosa ushindi katika mechi zao tatu zilizopita.
Katika mechi ya Kenya Police, City Stars walichukua uongozi kipindi cha kwanza kikielekea kukamilika kupitia Ezekiel Odera.
Hata hivyo, Mang’eni alifunga mabao mawili kipindi cha pili dakika za 60 na 61 mtawalia na kusaidia Kenya Police kupata ushindi wao wa nane wa msimu.?City Stars wapo nafasi ya 15 kwa alama 11.
Ratiba ya Alhamisi
Mechi zote zaanza saa tisa
Posta Rangers v Wazito (Kasarani Annex)
Subscribe our newsletter to stay updated