• Nairobi
  • Last Updated May 12th, 2024 6:50 AM
KINYUA KING’ORI: Wanaosababishia taifa hasara kwa miradi iliyokwama wachukuliwe hatua kali

KINYUA KING’ORI: Wanaosababishia taifa hasara kwa miradi iliyokwama wachukuliwe hatua kali

Maafisa serikalini, kuanzia kaunti hadi kitaifa, hawataacha ubadhirifu huu wa pesa za umma iwapo hawatakabiliwa vikali.

Kwanza, asiruhusiwe yeyote kuanzisha miradi bila kuwepo kwa taratibu mwafaka za ufuatiliaji na utathmini, ili kuhakikisha inakamilika na kuthibitishwa kuwa sawa kabla mwanakandarasi kulipwa.

Ufisadi umefanya viongozi na maafisa serikalini wakose kufuatilia namna miradi inatekelezwa.

Inadaiwa kuwa kampuni za baadhi ya viongozi mashuhuri ndizo hupewa kandarasi kutekeleza miradi mikubwa.

Ndiposa maafisa wa ngazi ya chini katika wizara husika wanashindwa kukagua ubora wa miradi hiyo.

Aidha, ushauri na kauli zao hupuuzwa iwapo kumetokea kazi duni, na kampuni hizo kuendelea kupokea malipo. Serikali ya Rais William Ruto na magavana wajitolee kupigana na ufisadi huu.

Wanakandarasi na kampuni zinazopora pesa za umma kwa kukosa kukamilisha miradi ipasavyo, zipigwe marufuku kuendesha miradi yoyote ya serikali. Nao wanasiasa, hususan walio na nyadhifa kuu serikalini, wasiruhusiwe kutumia vyeo vyao kujizolea zabuni kwa njia za mkato.

Wajibu wao wa kimsingi ni kulinda fedha za umma na kusaidia taifa kufanikisha miradi ya maendeleo itakayostawisha uchumi.

Hata hivyo, wao hutumia kila nafasi kujifaidi bila kujali ubora wa miradi kwa raia, ulafi ambao mwishowe ni ufujaji pesa na hasara.

Serikali isiidhinishe miradi isiyoleta mabadiliko ya kiuchumi kwa raia; lazima miradi iwe na manufaa halisi kwa jamii na taifa.

Zaidi, maafisa wanaoshirikiana na wanakandarasi wafisadi wanafaa kuwajibishwa kikamilifu kwa kuchukuliwa hatua kali kisheria ili kukomesha kabisa ulafi huo.

  • Tags

You can share this post!

Matano alia refa alipendelea Gor, Nzoia ikisalia juu

Familia ya Joho kortini ikilalama kuchafuliwa jina

T L