NA JOHN ASHIHUNDU
BEKI tegemeo wa AFC Leopards Kaycie Odhiambo atakuwa nje bila kucheza hadi msimu huu umalizike.
Odhiambo alijeruhiwa vibaya goti lake la kulia wakati wa mechi yao dhidi ya Wazito FC mnamo Aprili 18 ambapo kulingana na ripoti ya Daktari Patrick Ngusale, nyota huyo mwenye umri atakaa nje kwa miezi minne.
Ngusale ambaye ni mtaalamu wa viungo alisema itabidi staa huyo afanyiwe upasuaji baada ya kumalizika wiki tatu tangu aumie.
Odhiambo amejiunga na mastaa wengine wa Leopards Jaffary Owiti na Tedian Esilaba ambao wanauguza majeraha.
Mchezaji huyo wa zamani wa Hakati FC na Dandora Love alikuwa ameichezea Leopards mechi zote tangu ajiunga na kikosi hicho Novemba mwaka uliopita.
Kufikia sasa, Odhiambo ameifungia Leopards bao moja na kutoa pasi kadhaa zilizochangia mabao.
Akizungmza kuhusu kutukuwepo kwake, naibu kocha wa Leopards Tom Juma alisema kikosi kizima kimesikitika na kuumia kwake.
Bila Odhiambo kikosini Tusker ilivunja rekodi ya kutofungwa ya mechi 11 ya mabingwa hao mara 13 wa Ligi Kuu ya Kenya kwa mabao 2-1 katika mechi iliyochezewa MISC Kasarani.
“Tumesikitika kwa sababu amejeruhiwa wakati kiwango chake kilikuwa kimepanda kwa kiasi kikubwa,” alisema Juma.