• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Mwanatenisi Okutoyi aanza kuona matunda ya jasho lake, VasPro yammwagia nusu milioni

Mwanatenisi Okutoyi aanza kuona matunda ya jasho lake, VasPro yammwagia nusu milioni

Na GEOFFREY ANENE

NYOTA Angella Okutoyi ameeleza kufurahishwa na wadhamini kuanza kujitokeza kumpiga jeki baada ya kampuni ya kutoa huduma za kiteknolojia VasPro kumpa zawadi ya Sh500,000 mnamo Julai 20.

Okutoyi, 18, ambaye ni Mkenya wa kwanza kufika fainali ya shindano la Grand Slam na pia kushinda baada ya kunyakua taji la chipukizi la wachezaji wawili kila upande la Wimbledon akishirikiana na Mholanzi Rose Marie Nijkamp zaidi ya wiki moja iliyopita.

Siku moja baada ya hoteli za Serena kumpatia uanachama wa kupokea huduma za afya na urembo (Maisha Health & Spa), kampuni ya VasPro ilipokea nyota huyo katika afisi zake jijini Nairobi.

VasPro ilitambua juhudi za bingwa huyo wa zamani wa Kenya Open na Afrika Under-18 kwa kuweka Kenya kwenye ramani ya dunia kupitia tenisi.

“Sisi kama kampuni tunajivunia kushirikiana na Angella ambaye amethibitisha kuwa Kenya inaweza kutawala ulimwengu wa tenisi. Sifa zake, uthabiti wake, uvumilivu na matokeo yanaendana na maadili yetu kama kampuni,” alisema meneja wa ukuzaji wa biashara wa VasPro, Evans Mwika.

Okutoyi, ambaye amelelewa maisha yake yote na nyanya yake baada ya mama yake kuaga dunia mara alipojifungua pacha Okutoyi na Roselida Asumwa, alishukuru sana VasPro.

“Sikutarajia kabisa zawadi hii. Usaidizi huu wa kifedha utanisaidia katika tenisi yangu ya chipukizi ninapolenga juu na ninawaahidi nyote kuwa makubwa yaja,” alisema Okutoyi ambaye anajiandaa kwa shindano la Wanawake la Dola 15,000 za Amerika mjini Monastir, Tunisia mnamo Julai 25-31.

  • Tags

You can share this post!

GWIJI WA WIKI: Mathias Momanyi

Mikakati ya Uhuru kumpiga jeki Raila

T L