Na MASHIRIKA
NEWCASTLE United watamenyana na vigogo Paris St-Germain (PSG), Borussia Dortmund na AC Milan katika hatua ya makundi ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu huu wa 2023-24.
Kikosi hicho almaarufu Magpies, kilirejea katika soka ya UEFA muhula huu, kwa mara ya kwanza tangu 2002-03. Kitakuwa na kibarua kizito cha kuvaana na miamba watatu ambao wanajivunia kutinga fainali ya UEFA angalau mara moja katika kipindi cha miaka 16 iliyopita.
Wafalme mara 20 wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), Manchester United watapepetana na Bayern Munich, huku mabingwa watetezi wa UEFA, Manchester City, wakitiwa katika zizi moja na RB Leipzig ya Ujerumani.
Arsenal wamewekwa katika kundi moja na Sevilla huku Celtic kutoka Scotland wakikwaruzana na Atletico Madrid.
KUNDI A: Bayern Munich, Manchester United, FC Copenhagen, Galatasaray
KUNDI B: Sevilla, Arsenal, PSV Eindhoven, RC Lens
KUNDI C: Napoli, Real Madrid, Braga, Union Berlin
KUNDI D: Benfica, Inter Milan, Salzburg, Real Sociedad
KUNDI E: Feyenoord, Atletico Madrid, Lazio, Celtic
KUNDI F: Paris St-Germain, Borussia Dortmund, AC Milan, Newcastle United
KUNDI G: Manchester City, RB Leipzig, Red Star Belgrade, Young Boys
KUNDI H: Barcelona, Porto, Shakhtar Donetsk, Royal Antwerp
Mechi za hatua ya makundi zimeratibiwa kutandazwa kati ya Septemba 19 na Disemba 13, 2023 huku fainali ya UEFA ikitarajiwa kufanyika ugani Wembley, Uingereza, mnamo Juni 1, 2024.
Newcastle walijikatia tiketi ya UEFA msimu huu baada ya kuambulia nafasi ya nne kwenye msimamo wa jedwali la EPL mnamo 2022-23 chini ya kocha Eddie Howe.
Mtihani wao mgumu zaidi unatazamiwa kuwa dhidi ya Dortmund, PSG walionogesha fainali ya 2020 na mabingwa mara saba AC Milan waliokubali kichapo cha 1-0 kutoka kwa Man-City mnamo 2022-23.
Dortmund ya Ujerumani ilinyanyua taji la UEFA mnamo 1997 na walifuzu kwa fainali ya kivumbi hicho miaka 10 iliyopita.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO