• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
Norwich City warejea EPL kwa ajili ya msimu wa 2021-22

Norwich City warejea EPL kwa ajili ya msimu wa 2021-22

Na MASHIRIKA

NORWICH City wamepandishwa ngazi kushiriki Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa mara ya tano.

Hii ni baada ya washindani wao wakuu katika Ligi ya Daraja ya Kwanza nchini Uingereza (Championship), Brentford na Swansea City kutoshinda mechi zao za Jumamosi na hivyo kujiweka katika nafasi ya kutoweza kufikia Norwich ya kocha Daniel Farke kileleni.

Norwich almaarufu The Canaries, wanarejea EPL mwaka mmoja pekee baada ya kushushwa ngazi kwenye kivumbi hicho mnamo 2019-20.

Ni Watford pekee ambao kwa sasa wana alama nane zaidi ili kufikia Norwich ndio walio na uwezo finyu wa kunyima Norwich ubingwa wa taji la Championship kwa mara ya tatu. Norwich wamepanda ngazi kushiriki EPL mapema sana kwenye kampeni za Championship tangu 2004.

Kikosi hicho kilianza wikendi ya Aprili 17 kikihitaji angalau alama mbili pekee kutokana na mechi tano zilizosalia msimu huu ili kufuzu kwa gozi la EPL.

Hata hivyo, Norwich walijikatia tiketi ya kunogesha kipute cha EPL mnamo 2021-22 baada ya Brentford kuambulia sare tasa dhidi ya Millwall nao Swansea wakalazimishiwa sare ya 2-2 kutoka kwa Wycombe.

Katika kampeni za EPL mnamo 2019-20, Norwich walipoteza jumla ya mechi 13 kati ya 15 za mwisho na wakateremshwa ngazi hadi Championship baada ya msimu mmoja pekee kwenye kivumbi cha Ligi Kuu.

Japo vikosi huwa vigumu kwa vikosi vinavyoshuka ngazi kwenye EPL kurejea haraka kunogesha kivumbi hicho, Norwich walisalia watulivu na wakajenga imani kwa kocha wao Farke huku wakidumisha idadi kubwa ya wanasoka waliowategemea kwenye EPL mnamo 2019-20.

Ingawa walijizolea alama nne pekee kutokana na mechi nne za ufunguzi wa kipute cha Championship, Norwich walipaa hadi kileleni mwa jedwali baada ya kushinda Middlesbrough katika mchuano wao wa 12 mnamo Novemba.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Sheffield United wateremshwa daraja kutoka EPL hadi...

Kocha Hansi Flick kuagana rasmi na Bayern Munich mwisho wa...