• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:57 PM
NYOTA WA WIKI: Gabriel Jesus

NYOTA WA WIKI: Gabriel Jesus

NA GEOFFREY ANENE

GABRIEL Jesus ni mshambulizi matata wa Arsenal inayoshiriki Ligi Kuu nchini Uingereza.

Kinda huyu ametua kambini mwa Arsenal kwa kishindo.

Jesus alipuuza Real Madrid, Tottenham Hotspur na Chelsea akijiunga na wanabunduki kutoka Manchester City miezi miwili iliyopita, ameonekana kuwa mkombozi wa Arsenal mapema katika msimu huu wa 2022-2023.

Ana magoli matatu na kusuka idadi sawa ya pasi zilizokamilishwa.

Kifungamimba huyu, ambaye shujaa wake ni mshambulizi jagina Ronaldo Luis Nazario de Lima, alianza uchezaji kupitia soka ya mitaani akiwa na umri wa miaka mitano.

Alikuwa kiungo wa kati mwanzoni, lakini alipendezwa zaidi na majukumu ya ushambuliaji baada ya kuona Ronaldo akiibuka mfungaji bora kwa mabao manane kwenye Kombe la Dunia 2002.

Jesus alivutia timu kubwa mjini Sao Paulo alipofuma wavuni magoli 29 akichezea Anhanguera Associacao Paulista katika mashindano ya wachezaji wasiozidi umri wa miaka 15.

Miamba wa Palmeiras walimnyakua. Aliridhisha katika timu ya makinda kabla ya kupandishwa kuchezea timu ya watu wazima ya Palmeiras. Alipata jina la utani Little Neymar kwa weledi wake.

Alichangia mabao 12 na kusaidia Palmeiras kutoka mduara hatari wa kutemwa na kuwa mabingwa mwaka 2016.

Aliondoka Palmeiras akiwa ameifungia jumla ya mabao 21 na pasi sita zilizojaa nyavuni katika michuano 52.

Mabwanyenye wa Uingereza Manchester City walimsaini kwa Sh4.0 bilioni mwaka 2017.

Alijiunga na Arsenal kwa Sh6.2 bilioni. Yeye ni mchezaji anayekula mshahara mnene uwanjani Emirates; Sh36.8 milioni kila wiki.

Kimataifa, Jesus amechezea Brazil mara 56 na kufunga mabao 19.

  • Tags

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Mawakili wakongwe sasa wapishe chipukizi...

VITUKO: Penzi la Balotelli na Messina laingia doa akirudia...

T L