Na GEOFFREY ANENE
KENYA imezindua kikosi kitakachowania ubingwa wa mashindano ya tenisi ya Afrika ya Kundi la Tatu ya Billie Jean King Cup yatakayofanyika katika uwanja wa udongo wa Nairobi Club mnamo Juni 12-17.
Bingwa wa Rwanda Open wa kitengo cha mchezaji mmoja kila upande na Wimbledon ya chipukizi ya kitengo cha wachezaji wawili kila upande Angella Okutoyi ataongoza kampeni ya wenyeji.
Atashirikiana na Alicia Owegi na Cynthia Cheruto Wanjala na pia Roselida Asumwa, ambaye ni pacha wa Okutoyi. Melissa Mwakha na Stacy Yego wako katika kikosi cha akiba. Kocha Francis Rogoi ndiye nahodha asiyecheza.
Timu ya Kenya imepata motisha baada ya mfanyabiashara Ciiru Waweru kupatia kikosi hicho cha watu saba skafu na fulana zinazogharimu Sh100,000.
Kampuni ya Coca-Cola kupitia afisa wake wa mauzo Mitriam Limo pia ilitangaza kuwa itadhamini mashindano kwa kuwapa washiriki maji, soda na sharubati.
Kenya, Botswana, Burundi, Ghana, Mauritius, Morocco, Namibia, Nigeria, Ushelisheli, Tunisia, Uganda na Zimbabwe zitawania ubingwa wa Afrika. Atakayeibuka mshindi wa mashindano hayo ya mataifa 12 atapandishwa daraja hadi Europe/Africa Group II naye mvuta-mkia atashushwa hadi daraja la nne.