• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
PSG sasa wanahitaji alama moja kutokana na mechi tano ili kutawazwa wafalme wa Ligue 1

PSG sasa wanahitaji alama moja kutokana na mechi tano ili kutawazwa wafalme wa Ligue 1

Na MASHIRIKA

PARIS Saint-Germain (PSG) walilazimika kusubiri zaidi kabla ya kunyanyua taji la Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1) kwa mara ya nane chini ya kipindi cha miaka 10 baada ya washindani wao wakuu Marseille kutoka nyuma na kucharaza Nantes 3-2 mnamo Jumatano usiku.

Bila kujivunia huduma za Lionel Messi na Neymar Jr, PSG walistahili kufunga Angers angalau mabao manne kwa nunge ili kutawazwa wafalme wa Ligue 1 katika mchuano mwingine wa Jumatano. Lakini miamba hao walipokeza wenyeji wao kichapo cha 3-0 kupitia kwa Sergio Ramos na Kylian Mbappe aliyecheka na nyavu za Angers mara mbili.

Sasa alama moja pekee katika mechi itakayowakutanisha PSG na nambari saba Lens mnamo Aprili 23 itawavunia masogora wa kocha Mauricio Pochettino taji la Ligue 1 hata kama Marseille wataponda Reims kwa idadi kubwa ya mabao.

Kufikia sasa, PSG wanadhibiti kilele cha jedwali la Ligue 1 kwa alama 77 huku pengo la pointi 15 likitamalaki kati yao na nambari mbili Marseille ambao pia wamesakata mechi 33. Zimesalia mechi tano pekee kwa kampeni za Ligue 1 msimu huu kutamatika rasmi.

Neymar atakuwa sehemu ya kikosi kitakachotegemewa na PSG dhidi ya Lens. Nyota huyo raia wa Brazil alikosa mchuano dhidi ya Angers kutokana na marufuku ya kuonyeshwa kadi tano za manjano.

Messi, Marco Verratti na Presnel Kimpembe walikosa kunogesha mchuano uliokutanisha PSG na Angers kwa sababu ya majeraha. Angers wanakamata nafasi ya 14 kwa alama 34 sawa na Lorient.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Arteta akiri hajakuwa akimtendea Nketiah haki kwa kumlisha...

Man-City wapepeta Brighton na kurejea kileleni mwa jedwali...

T L