• Nairobi
  • Last Updated May 14th, 2024 10:01 PM
Real Madrid wachabanga Cadiz na kupaa hadi kileleni mwa jedwali la La Liga

Real Madrid wachabanga Cadiz na kupaa hadi kileleni mwa jedwali la La Liga

Na MASHIRIKA

REAL Madrid walichupa hadi kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) kwa alama sawa na Atletico Madrid baada ya kuwapepeta Cadiz 3-0 ugenini mnamo Jumatano.

Kabla ya kupulizwa kwa kipenga cha kuashiria mwanzo wa mchuano huo, idadi kubwa ya mashabiki wa Real Madrid waliandamana nje ya uwanja kulalamikia hatua ya Real kuwa sehemu ya kipute kipya cha European Super League (ESL) walichotarajia kushiriki kuanzia Agosti 2021.

Hata hivyo, tukio hilo halikuathiri uthabiti wa Real ambao chini ya kocha Zinedine Zidane, walipachika wavuni jumla ya mabao matatu katika kipindi cha kwanza.

Karim Benzema alicheka na nyavu mara mbili kabla ya kuchangia goli jingine lililojazwa kimiani na Alvaro Odriozola kupitia kichwa.

Real walishuka dimbani kwa minajili ya mechi hiyo wakitawaliwa na kiu ya kujinyanyua baada ya Getafe kuwalazimishia sare tasa katika gozi la La Liga mnamo Aprili 18, 2021.

Florentino Perez ambaye ni rais wa Real alikuwa mstari wa mbele kutetea mpango wa kuasisiwa kwa kivumbi cha ESL ambacho kwa mujibu wake, kilibuniwa mahsusi kwa lengo la “kuokoa soka”.

Real bado hawajatangaza kujiondoa kwao kwenye mashandiano ya ESL licha ya idadi kubwa ya klabu zilizohusishwa na kampeni hizo, zikiwemo sita kuu za Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), kujitoa.

Real ambao kwa sasa wanajiandaa kupepetana na Chelsea kwenye nusu-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA), wako katika vita vikali vya kukamilisha kampeni za La Liga msimu huu ndani ya orodha ya nne-bora na kufuzu kwa soka ya bara Ulaya muhula ujao.

Kwa sasa wanajivunia alama 70 sawa na Atletico ambao wana mchuano mmoja zaidi wa kusakata ili kufikia idadi ya mechi 32 ambazo zimetandazwa na Real na nambari tatu Sevilla waliowapiga Levante 1-0. Barcelona wanashikilia nafasi ya nne kwa alama 65 baada ya kutandaza jumla ya mechi 30 pekee.

MATOKEO YA LA LIGA (Aprili 21, 2021):

Cadiz 0-3 Real Madrid

Levante 0-1 Sevilla

Osasuna 3-1 Valencia

Real Betis 0-0 Bilbao

Alaves 2-1 Villarreal

Elche 1-1 Valladolid

You can share this post!

Polisi ashtakiwa kwa kuitisha hongo kutoka kwa mhudumu wa...

Spurs watoka nyuma na kusajili ushindi wa 2-1 dhidi ya...