Na MASHIRIKA
PARIS Saint-Germain (PSG) walipokea kichapo cha kwanza katika uwanja wao wa nyumbani tangu Aprili 2021 baada ya Rennes kuwapepeta 2-0 katika Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1).
Mechi hiyo ilikomesha rekodi ya kutopigwa kwa PSG katika mechi 35 za Ligue 1 ugani Parc des Princes na iliwapa Rennes jukwaa la kuwapepeta PSG mara mbili katika kampeni za ligi msimu huu wa 2022-23.
Wageni Rennes walifungua ukurasa wao wa mabao kupitia kwa Karl Toko Ekambi katika kipindi cha kwanza kabla ya Arnaud Kalimuendo kufunga la pili mwanzoni mwa kipindi cha pili.
Licha ya kichapo, PSG bado wanaselelea kileleni mwa jedwali la ligi la Ligue 1 kwa alama 66, saba kuliko nambari mbili Olympique Marseille waliokomesha rekodi ya kutoshindwa kwa Reims katika mechi 19 kwa kichapo cha 2-1.
Chini ya kocha Christophe Galtier, PSG wanapigiwa upatu wa kutwaa taji la Ligue 1 msimu huu ambalo litakuwa lao la 11 katika kipindi cha miaka 13 iliyopita.
Hadi waliposhuka dimbani kuvaana na Marseille, mara ya mwisho kwa Reims kupoteza mechi ya ligi ilikuwa Septemba 2022 ambapo AS Monaco iliwatandika 3-0.
Reims, wanaonolewa na kocha Will Still ambaye ni mzawa wa Ubelgiji na raia wa Uingereza, waliwekwa kifua mbele na fowadi Folarin Balogun anayewachezea kwa mkopo kutoka Arsenal.
Hata hivyo, juhudi hizo za Balogun zilifutwa na mshambuliaji wa zamani wa Arsenal, Alexis Sanchez, aliyecheka na nyavu mara mbili.
Rennes dicho kikosi cha tatu kuwahi kushinda PSG katika michuano miwili ya msimu mmoja wa Ligue 1 tangu umiliki wao utwaliwe na Qatar Sports Investments mnamo 2011. Rennes kwa sasa wanakamata nafasi ya tano jedwalini kwa alama nne nyuma ya nambari nne Monaco na pointi saba zaidi nyuma ya Lens wanaofunga mduara wa tatu-bora.
MATOKEO YA LIGUE 1 (Jumapili):
PSG 0-2 Rennes
Ajaccio 0-2 Monaco
Montpellier 2-1 Clermont
Nice 1-1 Lorient
Strasbourg 2-0 Auxerre
Troyes 2-2 Brest
Reims 1-2 Marseille
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO