• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:57 PM
GWIJI WA WIKI: Silvester Makau

GWIJI WA WIKI: Silvester Makau

Na CHRIS ADUNGO

KUNA idadi kubwa ya watu wanaojivunia mafao ya Kiswahili ulimwenguni.

Siri ya mafanikio yao imekuwa kufuata misukumo ya ndani ya nafsi zao hadi ndoto zao zikatimia.

Lenga kuwa bora katika chochote unachoteua kukishughulikia na umtangulize Mola katika kila jambo kwa kuwa ndiye mwelekezi wa hatua tunazozipiga maishani na kitaaluma.

Kufaulu katika jambo lolote kunahitaji mtu kuwa na bidii, maono na nidhamu ya kutenda mema bila kudhamiria malipo.

Huu ndio ushauri wa Bw Silvester Lunyiro Makau – mshairi shupavu, mwanadensi stadi na mwandishi mzoefu ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Idara ya Kiswahili katika Shule ya Msingi ya Manyole, eneo la Nambale, Kaunti ya Busia.

MAISHA YA AWALI

Makau alizaliwa Juni 30, 1978 katika kijiji cha Matawa, eneo la Mumias Magharibi, Kaunti ya Kakamega. Ndiye kitinda mimba katika familia ya watoto sita wa marehemu Josphine Chibete na marehemu Joseph Makau Wayugu aliyewahi kuwa mwalimu na askari wa magereza.

Makau ana mke, Bi Arnolda Lunyiro Wangatia, ambaye kwa sasa ni mwalimu wa Sayansi, Kiswahili na Hisabati katika Shule ya Msingi ya Nambale Urban, Busia. Mungu amewajalia watoto watatu – Emmanuel Murunga, Faith Anyango na Joseph Louise.

ELIMU

Makau alianza safari yake ya masomo katika chekechea ya Matawa mnamo 1986 chini ya mwalimu Adhiambo. Alijiunga baadaye na Shule ya Msingi ya Matawa hadi 1994. Akiwa huko, alikuwa mwanariadha hodari na mwanakundi wa 4K-Club.

Umilisi wake wa Kiswahili ulichangiwa pakubwa na waliokuwa walimu wake wa awali – Bw Zadock Ingutia (mstaafu), Tom Ambani (Shule ya Upili ya Mumias Muslim Boys, mchoraji hodari na msanii maarufu), Moses Karakacha (Shule ya Msingi ya Ebubaka) na Mwinamo Akunda ambaye hadi kustaafu kwake, alikuwa Mwalimu Mkuu katika Shule ya Msingi ya Matawa.

Hawa ni baadhi ya walimu waliompokeza malezi bora zaidi ya kiakademia na kumwamshia ari ya kukipigia chapuo Kiswahili baada ya kumshirikisha katika mashindano mbalimbali ya ulumbi, utambaji wa hadithi, usomaji wa habari, utunzi wa mashairi na uandishi wa insha.

Makau aliibuka mshindi wa mara kwa mara wa mapambano hayo katika shule nzima tangu akiwa mwanafunzi wa darasa la sita na akajizolea zawadi tele za haiba zilizompandisha katika majukwaa mbalimbali ya makuzi ya Kiswahili.

Mnamo 1995, alijiunga na shule ya seminari katika eneo la Mukumu, Kakamega kwa minajili ya masomo ya sekondari. Askofu Maurice Muhatia ambaye kwa sasa anahudumu katika Kaunti ya Nakuru alichangia pakubwa kuinua umilisi wa Makau katika Kiswahili baada ya kumtanguliza vyema katika usomaji wa riwaya ‘Shamba la Wanyama’.

Mnamo 1998 alihamia hadi Seminari ya Mama wa Mitume (Mother of Apostles Seminary) mjini Eldoret ambapo alikutana na mwalimu Musumba aliyemtandikia zulia zuri la Kiswahili.

Baada ya kukamilisha mtihani wa kuhitimu Hati ya Masomo ya Sekondari (KCSE) mnamo 1998, Makau alianza kufundisha katika Shule ya Msingi ya Matawa.

Alihudumu huko kwa kipindi cha mwaka mmoja kabla ya kuhamia Shule ya Msingi ya Mumias D.E.B. Katika shule hizi, alifundisha Kiswahili na masomo ya Sayansi, Zaraa na Biashara. Wengi wa wanafunzi wake walipasi mitihani yao kwa alama za juu.

Mnamo 2001, alijiunga na Chuo cha Mafunzo ya Ualimu cha Eregi, Kakamega na akawa kiongozi wa Y.C.S na mchezaji mashuhuri wa ngoma ya Isukuti hadi kiwango cha kitaifa. Anamkumbuka mwalimu wake wa Kiswahili Bw Fredrick Oduori Wafula aliyemtia ari ya kukipenda Kiswahili na kumpa mbinu na mikakati ya kulifunza somo lenyewe kwa ustadi zaidi hadi hatimaye akawa mwalimu bora.

Pia anatambua ukubwa wa mchango wa mwalimu Kizito Mugali – mnenaji mahiri wa Kiswahili ambaye kwa sasa ni mbunge wa Shinyalu, Kakamega. Ni Bw Mugali ndiye alimsadikisha Makau kwamba Kiswahili ni kiwanda kikubwa cha maarifa, ajira na uvumbuzi.

Baada ya kuhitimu kuwa mwalimu wa kiwango cha P1 mnamo 2002, Makau alianza kufundisha Kiswahili katika Shule ya Msingi ya Mumias Central kabla ya kuhamia Mumias Township kisha Imakale, Matungu.

Aliajiriwa na Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC) mnamo 2004 na kutumwa katika Shule ya Msingi ya Mwitoti, Mumias alikohudumu hadi 2007.

Alifundisha Mumias D.E.B kati ya 2008 na 2011 kisha kuhamia katika Shule ya Msingi ya Lureko, Mumias alikoamsha ari ya kuthaminiwa kwa Kiswahili miongoni mwa wanafunzi na walimu wenzake hadi 2014.

Kabla ya kuhamia Shule ya Msingi ya Manyole mnamo Disemba 2019, Makau aliwahi kufundisha katika Chuo cha Mafunzo ya Ualimu cha Eregi kati ya 2016 na Septemba 2019.

USOMI

Msukumo wa kujiendeleza kitaaluma ulimchochea Makau kujiunga na Chuo Kikuu cha Nairobi mnamo 2007 kusomea shahada ya ualimu (Kiswahili na Dini). Alifuzu mwishoni mwa 2011. Ari ya kukichapukia Kiswahili akiwa chuoni ni zao la kutangamana kwa karibu na wahadhiri wake Prof Rayya Timammy, Dkt Evans Mbuthia, Prof Iribe Mwangi, Dkt Mugambi, Dkt Ayub Mukhwana na Prof Kithaka Wa Mberia.

Mnamo 2014, alijiunga na Chuo Kikuu cha Kenyatta kusomea shahada ya uzamili katika Kiswahili. Miongoni mwa mikota wa lugha waliomlea zaidi kitaaluma akiwa huko ni Dkt Richard Wafula, Dkt Pamela Ngugi, Prof Ireri Mbaabu, Dkt Mwihaki, Dkt Timothy Arege, Dkt Onyango, Dkt Leonard Chacha, Dkt Wanjala, Dkt Miriam Osore na Prof Catherine Ndungo.

Anatazamia kufuzu Disemba 2021 baada ya kuwasilisha tasnifu “Uchanganuzi wa Uwiano wa Picha na Matini katika Fasihi ya Watoto katika Shule za Msingi za Kaunti ya Kakamega” chini ya usimamizi na uelekezi wa Dkt Ngugi.

Anawashukuru Bw Mokono (mwalimu wa Kiswahili), Bw Wafula Oduori (Mtahihi Mkuu wa Baraza la Mitihani la Kenya) na Bw Mirikau Suleiman (mwandishi wa vitabu vya vyuo vya walimu) kwa uelekezi wao wa mara kwa mara uliochangia matokeo bora ya wanafunzi wake katika mitihani ya kitaifa ya PTE.

UANDISHI

Makau ameandika na kuchapishiwa makala mbalimbali ya kitaaluma. Miongoni mwa kazi zake ni ‘Lugha na Mtoto’, ‘Lugha ya Pili’, ‘Mfumo wa 8-4-4’, Mtaala wa Umilisi (CBC)’, ‘Nafasi ya Kiswahili katika Ukadiriaji wa Mtaala wa Umilisi Gredi ya 3’, ‘Jinsi Mtaala wa Umilisi (CBC) Hujenga Stadi za Kiswahili’, ‘Ni Mtihani ama ni Mkadiriaji wa Mtaala wa Umilisi (CBC)?’ na ‘Ufunzaji wa Sauti ‘t’ na ‘d’ kwa Kutumia Mtindo wa Tusome na CBC’.

Kwa sasa anaandaa kitabu cha hadithi kwa wanafunzi wa kiwango Gredi 2 kiitwacho ‘Njiwa’. Mnamo 2019, Makau alitunga shairi ‘IOM Japan Hoyee!’ lililokaririwa na wanafunzi wa Shule ya Upili ya Kwale Girls chini ya uelekezi wa mwalimu wao Bi Zainab Ramadhan kwa nia ya kuwashukuru wafadhili wa shule hiyo.

JIVUNIO

Makau anajivunia kufundisha idadi kubwa ya wataalamu na wasomi ambao kwa sasa wanashikilia nyadhifa za hadhi katika sekta mbalimbali za maendeleo ndani na nje ya ulingo wa Kiswahili.

Baadhi yao ni Anne Waswa ambaye ni mhadhiri wa Kemia nchini Amerika, Dkt Rebecca Wanga, mwalimu Bonface Otuko wa Shule ya Upili ya Matawa, mwalimu Magaret Auma Were wa Shule ya Sekondari ya Lufumbo, mwalimu Martha wa Kaunti ya Nyeri na mwalimu Isabella Wangatia wa Shule ya Upili ya Khayo, Busia.

Makau anamstahi mno Bi Alice Ghettu – mwalimu wa Kiswahili na Sayansi Kimu ambaye amesimama naye kwa hali na mali ili kufanikisha kila hatua anayoipiga kitaaluma.

Anapojitahidi kufikia upeo wa taaluma yake na kuweka hai ndoto zake za kuwa profesa wa Kiswahili, mwandishi maarufu, mhariri stadi na mwanadiplomasia mashuhuri, Makau anajivunia kuwa kiini cha motisha ambayo kwa sasa inawatawala walimu wengi anaoshirikiana nao katika jitihada za kukitetea Kiswahili.

You can share this post!

Riadha za Nusu-Marathon Duniani 2022 zaahirishwa kwa miezi...

Wakazi walaumiwa kuficha al-Shabaab

T L