• Nairobi
  • Last Updated May 12th, 2024 8:50 AM
Salah ataka Liverpool wamfanye sogora ghali zaidi wa EPL ili asalie ugani Anfield

Salah ataka Liverpool wamfanye sogora ghali zaidi wa EPL ili asalie ugani Anfield

Na MASHIRIKA

FOWADI matata raia wa Misri, Mohamed Salah, amewataka Liverpool kumpa mshahara wa hadi Sh78 milioni kwa wiki ndipo arefushe muda wa kuhudumu kwake uwanjani Anfield.

Salah, 29, tayari ni miongoni mwa wanasoka wanaodumishwa kwa ujira wa juu zaidi kambini mwa Liverpool. Iwapo masharti yake yatazingatiwa na waajiri wake, basi atakuwa mchezaji anayelipwa mshahara wa juu zaidi katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

Mgongo wa Salah utasomwa kwa karibu sana na mfumaji raia wa Ureno, Cristiano Ronaldo ambaye sasa hutia mfukoni Sh75 milioni kwa wiki ugani Old Trafford tangu aagane na Juventus ya Italia na kutua Manchester United.

Salah ambaye sasa hutia mfukoni Sh31 milioni kwa wiki, angali na miaka miwili pekee katika mkataba wake na Liverpool. Kocha Jurgen Klopp analenga kushawishi Liverpool kurefusha muda wa Salah na kuzima tetesi nyingi zinazohusisha sogora huyo na uwezekano wa kuhamia Paris Saint-Germain (PSG) au Real Madrid wanaohemea pia chipukizi Kylian Mbappe.

Kufikia sasa, Liverpool tayari wamefaulu kushawishi vigogo Virgil van Dijk, Alisson Becker na Jordan Henderson kutia saini kandarasi mpya.

Liverpool ni miongoni mwa vikosi vya EPL ambavyo havikujishughulisha sana katika soko la uhamisho wa wachezaji muhula huu. Miamba hao walijinasia huduma za sogora mmoja pekee – beki Ibrahima Konate aliyeagana na RB Leipzig ya Ujerumani kwa Sh5.6 bilioni.

Salah aliyeongoza Misri jana kuvaana na Gabon kwenye mechi ya kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2022, amekuwa tegemeo kubwa la Liverpool tangu asajiliwe kwa Sh5 bilioni kutoka AS Roma ya Italia.

TAFASIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Lukaku afunga bao lake la 67 katika mechi ya 100 ndani ya...

Makanisa yakataa Ruto