• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
SERIE A: Martinez afunga mabao matatu na kusaidia Inter Milan kuponda Crotone 6-2

SERIE A: Martinez afunga mabao matatu na kusaidia Inter Milan kuponda Crotone 6-2

Na MASHIRIKA

FOWADI Lautaro Martinez alifunga mabao matatu na kusaidia waajiri wake Inter Milan kupepeta Crotone 6-2 katika Ligi Kuu ya Italia (Serie A) mnamo Jumapili.

Ushindi huo wa Inter wanaotiwa makali na kocha Antonio Conte uliwawezesha kuwapita watani wao AC Milan na kutua kileleni mwa jedwali kwa alama 36. Milan wanaonolewa na kocha Stefano Pioli walitarajiwa kuvaana na limbukeni Benevento katika mchuano mwingine wa Serie A baadaye Januari 3, 2021.

Romelu Lukaku alifunga bao lake la 50 akivalia jezi za Inter Milan waliojipatia mabao mengine kupitia wanasoka Achraf Hakimi na Luca Marrone aliyejifunga.

Niccolo Zanellato aliwafungulia Crotone kunako dakika ya 12 kabla ya penalti ya kiungo Vladimir Golemic katika dakika ya 36 kusawazisha na kufanya mambo kuwa 2-2.

Goli lililofumwa wavuni na Lukaku lilikuwa lake la 12 katika kampeni za Serie A muhula huu. Nyota huyo wa zamani wa Everton na Manchester United kwa sasa anaongoza orodha ya wafungaji bora wa Serie A kufikia sasa msimu huu kwa pamoja na Cristiano Ronaldo wa Juventus.

“Ni ushindi muhimu ambao unastahili kutuaminisha hata zaidi. Ni matarajio yetu kwamba kikosi kitaendeleza ubabe huo katika michuano mingi ijayo na kuweka hai matumaini ya kutwaa taji la Serie A kwa mara ya kwanza tangu 2010 baada ya kubanduliwa mapema kwenye soka ya Klabu Bingwa Ulaya,” akasema Conte ambaye pia amewahi kunoa klabu ya Chelsea na timu ya taifa ya Italia.

  • Tags

You can share this post!

Leicester City wacharaza Newcastle United na kuingia ndani...

Arsenal kuwatoa chipukizi Willock, Nketiah na Reiss-Nelson...