Na GEOFFREY ANENE
KENYA Shujaa wametunukiwa na serikali Sh3 milioni kwa juhudi zao kwenye Kombe la Afrika la raga ya wachezaji saba kila upande ambapo waliibuka wafalme baada ya kunyuka Afrika Kusini 17-12 katika fainali jijini Harare, Zimbabwe mnamo Septemba 17.
Vijana wa kocha Kevin ‘Bling’ Wambua walirejea nyumbani Jumatatu usiku na kusababisha shughuli za kawaida kusimama katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) jijini Nairobi wakishangiliwa na mashabiki.
Mapema Jumanne, Waziri wa Michezo Ababu Namwamba amekutana na kikosi hicho kilichojumuisha wachezaji sita wapya na sita wazoefu pamoja na maafisa wake wakiongozwa na Wambua na viongozi wa Shirikisho la Raga Kenya (KRU) akiwemo mwenyekiti Sasha Mutai.
“Huwa hatuzitunuku timu zikishiriki mashindano ya kuingia Olimpiki, lakini kwa sababu mlifanya makubwa kwa kuangusha timu zote wakiwemo miamba Afrika Kusini katika fainali, Rais William Ruto ameahidi mpokee zawadi ya Sh3 milioni,” akasema Ababu akitoa hundi kwa timu hiyo katika dhifa ya chakula cha asubuhi iliyogharimiwa na wizara hiyo katika hoteli ya kifahari ya Weston jijini Nairobi.
Ababu amesema kuwa kila mchezaji aliyekuwa Harare atatia mfukoni Sh200,000 nao maafisa sita wa benchi ya kiufundi watapata Sh100,000 kila mmoja.