• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
Vihiga Queens watinga nusu fainali Dimba la CECAFA

Vihiga Queens watinga nusu fainali Dimba la CECAFA

NA TOTO AREGE

BAO la mshambulizi Bertha Omitta kunako dakika ya 36 wakicheza dhidi ya AS Kigali ya Rwanda, lilitosha kuwapa Vihiga Queens tiketi ya kuingia kwenye nusu fainali ya Kombe la Baraza la Mashirikisho ya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).

Mechi hiyo ilipigwa ugani MTN Omondi nchini Uganda.

Omitta ambaye alianza kwenye mechi kuchukua nafasi ya mshambilizi Tumaini Nafula, kwenye mechi ya awali dhidi ya New Generation ya Zanzibar, alianza kutoka benchi na kucheza dakika 15 pekee za mwisho.

Kwenye mechi hiyo ilikuwa  ya kwanza ya hatua ya makundi, Vihiga walitoka nyuma na kuandikisha ushindi wa  3-1.

Wababe hao wa Ligi Kuu ya Wanawake nchini (KWPL), wanaongoza kwenye kundi B na alama sita sawa na JKT ya Tanzania lakini wanatofautiana kwa mabao.

Kwenye mechi ya mapema jana Jumatano katika uwanja uo huo, JKT walioandikisha ushindi kwenye mechi ya pili dhidi ya New Generation.

Kulingana na kocha wa Vihiga Charles Okere, ushindi ulitokana na wasichana wake kufuata maagizo uwanjani.

“Kongole kwa wasichana kwa kuwa, walifuata maagizo kuanzia mwanzo hadi mwisho. Haya yote yanatokana na mazoezi mazuri ambayo tumekuwa nayo. Wapinzani wetu pia ningependa kuwapa kongole kwa kuonyesha mchezo mzuri. Hii pia ni timu nzuri manake walitupa wakati mgumu,” alisema Okere.

Mara ya mwisho Vihiga kutinga nusu fainali ni mwaka 2021 ambapo waliinyorosha New Generation 8-0 katika uwanja wa Nyayo jijini Nairobi. Katika mashindano hayo, walitwaa ubingwa wa CECAFA.

Mwaka 2022, wababe hao wa KWPL hawakuweza kutetea ubingwa wao nchini Tanzania kutokana na Kenya kufungiwa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

Vihiga watacheza mechi ya mwisho ya hatua ya makundi dhidi ya JKT wikendi hii katika uwanja uo huo.

  • Tags

You can share this post!

Neymar alitaka kasri la vyumba 25 kabla ya kuhamia klabu ya...

Chania High yapokea Sh10 milioni kutoka kwa Rais

T L