• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Vipusa wa Arsenal wapata kocha mpya

Vipusa wa Arsenal wapata kocha mpya

Na MASHIRIKA

KLABU ya wanawake ya Arsenal imempokeza mikoba kocha Jonas Eidevall ambaye ameagana rasmi na Rosengard ya Uswidi.

Mkufunzi huyo mwenye umri wa miaka 38 aliongoza Rosengard kutinga robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo 2020-21.

Anajaza pengo la Joe Montemurro aliyekatiza uhusiano wake na Arsenal mwishoni mwa msimu wa 2020-21 baada ya miaka minne.

Eidevall ambaye aliwahi kuwa msaidizi wa kocha Henrik Larsson kambini mwa Helsingborgs nchini Uswidi, aliongoza Rosengard kutia kapuni mataji matatu ya Ligi Kuu ya Uswidi baada ya kuondoka kambini mwa Lunds BK alikoanzia taaluma yake ya ukufunzi akiwa na umri wa miaka 23.

Larsson ni mchezaji wa zamani wa Celtic, Barcelona na Manchester United.

Baada ya kuhudumu kambini mwa Lunds BK kwa miaka mitatu na nusu na kutwaa taji la Ligi ya Daraja la Kwanza, alihamia Rosengard na kuongoza kikosi hicho mataji ya Ligi Kuu mnamo 2013 na 2014.

Alirejea Rosengard mnamo 2018 na kushindia kikosi hicho taji la Swedish Cup mnamo 2019.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Serikali kuhakikisha wakazi wa mitaa ya mabanda wanapata...

Thierry Neuville amwaga Sh257,000 milioni kusaidia ndovu na...