Na MASHIRIKA
KOCHA wa Liverpool Jurgen Klopp amesema kuwa difenda wake wa kutegemewa, Virgil van Djik yuko tayari kusakata kabumbu baada ya kupona jeraha la goti.
Van Djik, mzawa wa Uholanzi amekuwa akiuguza jeraha hilo tangu Oktoba mwaka jana, alilopata ugani Goodison Park baada ya kugongana na mlinda lango wa Everton Jordan Pickford.
Mabeki wengine; Joe Gomez, Joel Matip na Alexander-Arnold pia watarejea baada ya kupona majeraha waliyokuwa wakiuguza kwa muda.
Liverpool walipitia wakati mgumu baada ya kuumia kwa wachezaji hawa, hali iliyosababisha wapoteze uthabiti wa kutetea taji la EPL, ambalo lilinyakuliwa na mahasimu wao Manchester City.
Katika taarifa kwenye tovuti ya klabu hiyo, Klopp alieleza kuwa Van Djik na Gomez wanaendelea na vipimo vya matibabu na watakaguliwa kwa muda wa wiki mbili ili kuhakikisha wamepona kikamilifu.
“Wanaendelea na vipimo vyao na ni matumaini yangu kuwa wataruhusiwa kucheza,” alisema.
Matip aliumia misuli ya muundi Februari na bado anaendelea kupata afueni.
Arnold alirejea kwenye kikosa cha Uingereza mwishoni mwa dimba la Euro, lakini akalazimika kuondoka baada ya kuumia pajani kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya Austria.
Klopp alisisitiza kwamba Matip atarejea karibuni, huku Arnold akitarajiwa kuzidi kukaguliwa kwa siku tano au sita zaidi.
TAFSIRI NA: NDUNGI MAINGI