NA PATRICK KILAVUKA
ALIWAKILISHA kanda ya Nairobi katika mashindano ya Michezo ya Riadha kwa Shule za Msingi kitaifa ambayo yaliandaliwa katika uga wa Ole Ntimama, Narok kama bingwa wa mbio za mita 100 na kikosi cha mita 4×100.
Anazamia kukimbia kama kielelezo Ferdinand Omanyala ambaye ni bingwa Afrika na Jumuiya ya Madola, na ambaye hata juzi alinyakua taji la Absa Kip Keino Continental Tour ugani Kasarani mnamo Jumamosi iliyopita kwa muda wa sekunde 9.84.
Vivian Moraa,13, ni mwanafunzi wa gredi ya saba shule ya msingi na World Hope Academy, Kawangware, Nairobi.
Yeye ni kitinda mimba katika familia ya watoto watatu wa Bw Leonard Omwenga na Bi Eunice Khavai.
Alianza mbio akiwa gredi ya pili ambapo alikuwa na anaelekezwa na mwalimu wake Veronicah Otieno.
Anasema alikuwa anamhimiza kuendelea kushiriki katika michezo kila uchao kama njia ya kukuza talanta na kujiimarisha afya.
Hata hivyo, alijiunga pia na mradi wa Awana ambao uliendelea kumchochea zaidi kujikuza kispoti.
Kujiandaa mwaka huu kwa mashindano ya Michezo ya Riadha Shule za Msingi, anasema alijifunga kibwebwe akiamini kwamba, atafika kitaifa majaliwa.
Dua yake ilijibiwa pale ambapo alinogesha mbinu za mchezo huu kwa kukimbia mbio za umbali wa mita 100.
Katika mashindano ya Zoni ya Riruta yaliyoandaliwa Kawangware, aliibuka nambari wani kwa kusajili muda bora wa sekunde 11.80.
Alipanda ya Kaunti ndogo ya Dagoretti Mashariki na kuwa kidedea kwa muda wa sekunde 11.96 ambayo yaliandaliwa shule ya sekondari ya Dagoretti High.
Baada ya kujifua zaidi chini wa kocha Geoffrey Wesonga, mwalimu wa michezo shuleni Raymond Shirandula na wadau wengine shuleni, alipata muda bora zaidi katika mita 100 wa sekunde 12.60 katika mashindano ya Jimbo la Nairobi yaliyofanyika shule ya msingi ya Moi Forces, Nairobi.
Alichaguliwa kupeperusha bendera ya jimbo la Nairobi kitaifa.
Alipambana ukucha kwa jino, japo aliibuka wa saba bora kwa muda sekunde 12.96 kitaifa.
Alishiriki pia katika kikosi cha mbio za kupokezana vijiti za 4×100 Kanda ya Nairobi na kumaliza saba bora kitaifa kwa muda waka sekunde 13.76.
Alituzwa cheti cha ushindi mbio za 100 kanda ya Nairobi na vyeti vya kushiriki mita hizo na 4×100 kupokezana vijiti kitaifa.
Mwanariadha chipukizi Moraa anasema alikuwa anafanya mazoezi kila siku kuimarisha misuli.
Pia, alikuwa anajaribu kadri awezavyo kujiepusha na kukula vyakula vyenye mafuta mengi kwa kuzingatia lishe bora.
Changamoto yake ilikuwa kukimbia bila viatu vya kukimbia lakini baada ya kufanya vizuri, shule ilijitolea kumnunulia.
Hapo ndipo, alipata mori kutokana na utambuzi wa juhudi zake katika mchezo huo.
Katika masomo, mwalimu wake Moses Ayodi anasema ni mwanafunzi ambaye anapenda masomo na anapata alama juu.
Mbali na kujikasa masomo akinuia kusomea uhandisi wa maroboti huku akipania kuwa mwanariadha.
Mtimkaji Moraa anadokeza kwamba, anayachota mambo mengine kuhusu riadha kupitia mitandao ya kijamii kama njia ya kujua jinsi wanariadha wengine wanavyojiimarisha.
Kama hasomi wala hashiriki riadha, mkimbiaji huyu hucheza soka au mpira wa vikapu.
Ushauri wake ni kwamba, ukitaka kuwa mkimbiaji, anza pole pole, jitume na utafika ngazi za juu.