• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
Wanaraga wa Kabras Sugar wavunja rekodi ya KCB kutoshindwa ligini

Wanaraga wa Kabras Sugar wavunja rekodi ya KCB kutoshindwa ligini

Na GEOFFREY ANENE

MABINGWA watetezi Kabras Sugar wamevunja rekodi ya wenyeji KCB kutoshindwa baada ya kuwalima 31-23 uwanjani KCB Ruaraka mjini Nairobi kwenye Ligi Kuu ya raga nchini (Kenya Cup), Jumamosi.

Wanasukari wa Kabras, ambao sasa wamejiweka pazuri kuandaa fainali ya dimba hilo la klabu 12 wakitamatisha msimu kileleni, waliongoza 16-0 kupitia kwa pointi kutoka kwa Ntabeni Dukisa (goli la alama tatu, mkwaju na penalti mbili) na Jone Kubu (mguso). Wanabenki wa KCB walipata alama zao za kwanza wakati Darwin Mukidza alitinga penalti na kukata mwanya huo hadi 16-3.

Uongozi wa Kabras ulipunguzwa zaidi hadi 16-10 baada ya KCB kupata mguso kutoka kwa Samuel Asati na mkwaju kutoka kwa Mukidza.

Kabras kutoka kaunti ya Kakamega ilijipata chini 17-16 mapema katika kipindi cha pili baada ya Mukidza kupachika mkwaju wa mguso wa nahodha Curtis Lilako.

Hata hivyo, Dukisa alirejesha Kabras kifua mbele 19-17 alipoongeza penalti. Uongozi wa Kabras pia ulidumu muda mfupi kwani KCB ilichupa mbele 20-19 baada ya kupata penalti, Mukidza akifuma vyema katikati ya milingoti.

Mukidza aliongeza penalti iliyoimarisha uongozi wa KCB hadi 23-19, lakini miguso miwili ukiwemo mmoja kutoka kwa Kubu pamoja na mikwaju miwili ilitosha kupatia Kabras ushindi muhimu.

Katika matokeo mengine, Menengai Oilers waliteketeza Monks ya Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afrika Mashariki (CUEA) 55-0, Leos ya Chuo Kikuu cha Strathmore ilifufua matumaini ya kukwepa kuangukiwa na shoka iliponyuka Mean Machine ya Chuo Kikuu cha Nairobi 34-10 nayo Blak Blad ya Chuo Kikuu cha Kenyatta ikazima Chuo Kikuu cha Masinde Muliro 15-8. Nakuru ilinyamazisha ‘madeejay’ wa Homeboyz 30-8 nayo Mwamba ikasalimu amri ya Kenya Harlequin 22-11.

Kwingineko, timu ya taifa ya raga ya wachezaji saba kila upande ya Kenya almaarufu Shujaa, itaelekea Amerika ya Kaskazini siku ya Jumapili kwa duru mbili zijazo za Raga za Dunia mijini Los Angeles na Vancouver.

  • Tags

You can share this post!

Mwendeshaji bodaboda ashtakiwa kwa kujifanya mke wa Gachagua

WALIOBOBEA: Pandashuka, mafanikio ya Kenyatta katika siasa

T L