NA WANDERI KAMAU
IDADI kubwa ya wawaniaji huru wa urais imewafanya kuteua alama za kujitambulisha ambazo baadhi ni za vyama vilivyopo.
Kwa mfano, mwaniaji urais George Munyottah Kamau anatumia alama ya taa, ilhali alama iyo hiyo imekuwa ikitumika kwa muda mrefu na chama cha Democratic Party (DP).
Kulingana na wakili Kahihia Murache, kwa mwaniaji huru yeyote kuruhusiwa kutumia alama yeyote ile, lazima awe ametimiza mahitaji ya Katiba.
“Kipengele 85 cha Katiba kinatoa ufafanuzi kuhusu mazingatio ambayo mwaniaji huru anapaswa kutimiza ili kuruhusiwa kuwania wadhifa wowote, iwe udiwani, ubunge, useneta, ugavana au urais. Moja ya hitaji hilo ni kuwa lazima alama atakayotumia isiwe inatumiwa na mtu mwingine,” akasema wakili huyo.
Licha ya utata huo, mwenyekiti wa IEBC, Bw Wafula Chebukati anashikilia kuwa hatua ya tume kutoa orodha ya wawaniaji hao inaashiria kuwa wametimiza kanuni zote zinazohitajika.
“Uchapishaji wa majina ya wawaniaji huru na alama wanazotumia ndiyo hatua ya mwisho kuonyesha kuwa imeridhishwa nao,” akasema, alipohutubu majuzi mjini Naivasha.
Hata hivyo, mawakili wanasema chama ama mwaniaji huru ana haki kwenda mahakamani ikiwa atahisi kuwa alama yake imetumiwa na mwaniaji mwingine bila kibali chake.
Wengine wametumia alama ambazo maana yake inaweza kukanganya kama vile kobe, ambaye anafahamika kwa kutembea kwa mwendo wa polepole.