Azimio yaonya polisi kuhusu maandamano
JUSTUS OCHIENG Na CECIL ODONGO
VIONGOZI wa Azimio la Umoja wamewaonya polisi kuwa watawajibikia vitendo vyao wenyewe iwapo watawavamia raia wakati wa maandamano yanayopangwa na muungano huo wa upinzani jijini Nairobi kesho Jumatatu.
Vinara wa Azimio, wakiongozwa na Bw Raila Odinga, wamewaonya polisi kwamba, huenda wakajipata mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), jijini The Hague, Uholanzi.
Kwenye mahojiano ya kipekee na Taifa Jumapili, aliyekuwa Waziri wa Ulinzi, Bw Eugene Wamalwa aliwatahadharisha polisi dhidi ya kuvunja sheria, akisema kuwa ICC inafuatilia yanayojiri nchini na kila polisi atawajibikia matendo yake kibinafsi.
Aliwakumbusha kuhusu kesi za ICC ambapo aliyekuwa Kamishina wa Polisi Hussein Ali alishtakiwa kuhusiana na mauaji yaliyotokea baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2007.
“Wewe polisi ambaye atamuua mwandamanaji utawajibika kivyako. Ukimuua au kumjeruhi Mkenya mnamo Jumatatu, wewe ndiye utahusika. Ikulu ni Nyumba ya watu. Wafanyabiashara wa Nyamakima hivi majuzi walijitokeza kwa wingi na kuandaa maandamano hadi afisi ya Naibu Rais kisha wakawasilisha malalamishi yao,” akasema Bw Wamalwa.
“Vivyo hivyo, wakazi wa Kisumu waliwasilisha malalamishi yao kwa Kamishina wa Kaunti. Iwapo, Wakenya wangetaka kuelekea Ikulu mnamo Jumatatu kuwasilisha malalamishi yao kwa William Ruto, basi wapo huru kufanya hivyo,” akaongeza.
Kinara huyo wa DAP-K alisema kutembelea Ikulu ya Nairobi si hatia na iwapo itatokea hivyo, basi polisi wanastahili kuwaruhusu waandamanaji waelekee ikulu ili wazungumziwe na Rais.
“Raia hawahitaji idhini ya Ruto ili kuandaa maandamano. Polisi wanastahili kuwasindikiza hadi ikulu wahutubiwe na Rais,” akasema.
Kauli ya Bw Wamalwa kwamba ICC inafuatilia matukio nchini ilitolewa wakati korti hiyo imetoa kbali cha kukamatwa kwa Rais wa Urusi, Vladimir Puttin kutokana na mauaji na ukiukaji wa haki za kibinadamu nchini Ukraine.
Maandamano hayo yanatokana na lalama kuhusu kupanda kwa gharama ya maisha, kusaka haki kuhusiana na uchaguzi mkuu uliopita na uteuzi unaoendelea wa makamishina wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) ambao wanadai unaendeshwa kwa njia ya ubaguzi.
Serikali imeripotiwa kuweka mikakati kabambe ya kukabiliana na waandamanaji na kuwazuia kuvuruga shughuli za kawaida katikati mwa jiji la Nairobi. Maafisa wa vikosi mbalimbali vya polisi wako ange kuzuia visa vyovyote vya utovu wa usalama.
Jana Jumamosi, wanachama 50 wa chama cha kitaifa cha wanafunzi wa vyuo vikuu (KUSO) walikamatwa na kuzuiliwa katika kituo cha polisi cha Central, Nairobi. Hii ni baada ya polisi kuvamia kikao chao na waandishi wa habari katika Chester House, Nairobi ambapo walielezea mikakati yao ya kushiriki kwenye maandamano yaliyoitishwa na muungano wa Azimio mnamo Jumatatu.
Na wakizungumza katika kaunti ya Kiambu mnamo Ijumaa, vinara wenza Kalonzo Musyoka, Martha Karua, na aliyekuwa Mwaniaji wa Urais Profesa George Wajackoya, waliwaonya Rais na Inspekta Jenerali wa Polisi Japheth Koome kuwa, iwapo polisi watawavamia waandamanaji, basi ni wawili hao na polisi husika watawajibika.
WAFUASI
“Askari msije mkatumiwa Jumatatu. Nataka mjue duniani hata Wafaranasa, Israeli na Belarus wanaandamana. Msitumiwe vibaya ilhali maandamano ni haki ya raia ya kikatiba,” akasema Bw Musyoka akiwahutubia wafuasi wa Azimio eneo la Ruaraka.
Seneta wa Narok Ledama Ole Kina pia aliwaeleza polisi kwamba, maadili yao ya kazi haiwaruhusu kukiuka haki za raia na kuwataka wasitumie maandamano ya Jumatatu kuwaua raia hata wakiamrishwa kufanya hivyo.
“Raila amewapigania wananchi kwa miaka mingi na sasa wananchi wameamua kujipigania wenyewe. Kama unajijali, jitokeze Jumatatu kwa sababu serikali hii imeonyesha haiwajali. Polisi wasikubali kutumiwa vibaya kuwaadhibu raia wanaopigania haki,” akasema Seneta huyo.
Akizungumza mjini Nyeri, Bw Gachagua alisema maandamano hayo ya upinzani yanalenga kuharibu biashara zinazomilikiwa hasa na jamii ya Wakikuyu.
Jijini Nairobi, baadhi ya wafanyabiashara walielezea hofu ya kutofungua biashara zao Jumatatu.
Madereva wa magari ya uchukuzi walieleza Taifa Jumapili kwamba, hawatadhubutu kuweka magari yao barabarani licha ya upinzani kusisitiza kuwa maandamano hayo yatakuwa ya amani.
“Hiyo siku sipo kazini kwa sababu siwezi kuhatarisha gari langu. Mimi nafahamu yaliyotokea kwenye maandamano yaliyofanyika miaka ya nyuma,” akasema mmoja wa madereva wa Utimo, magari ambayo husafirisha abiria kutoka Nairobi hadi mtaani Umoja.
Vijana katika mitaa mbalimbali kama Umoja, Kibera na Mathare nao waliahidi kushiriki maandamano hayo huku wakidai serikali imeghairi nia kuhusu ahadi ilizotoa wakati wa kampeni.
Mjini Kisumu, wanasiasa wa ODM waliahidi kuwasafirisha wafuasi wao hadi jijini Nairobi kushiriki maandamano hayo. Wakati wa mkutano wa kisiasa katika uwanja wa Ahindi, Siaya wiki hii, wabunge wa ODM na Gavana James Orengo waliahidi kukodisha mabasi ya kusafirisha wafuasi wao hadi Nairobi.
“Tunakuja Nairobi, baadhi watafika Jumapili asubuhi na wengine jioni. Hata wenzetu kutoka Magharibi wanakuja huko. Sisi kama viongozi tunahusika pia na safari hizo,” Diwani wa wadi ya Milimani, Kisumu Seth Kanga maarufu kama Adui Nyang’ akaeleza Taifa Jumapili.
Na jana Jumamosi, Naibu Rais aliendelea na ziara zake katika ngome zake za kisiasa eneo la Mlima Kenya ambapo alihimiza wenyeji kususia maandamano hayo ya Jumatatu.
Kando na Kenya, maandamano kesho Jumatatu dhidi ya serikali yataendelea Afrika Kusini na Tunisia.
Next article
‘Maandamano yetu si ya fujo’