• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:55 AM
‘Maandamano yetu si ya fujo’

‘Maandamano yetu si ya fujo’

NA JUSTUS OCHIENG

HUKU Muungano wa Azimio la Umoja ukijiandaa kuongoza maandamano kesho Jumatatu.

Taifa Jumapili ilikuwa na mahojiano na aliyekuwa Waziri wa Ulinzi Eugene Wamalwa kuhusu suala hilo.

Nini mpango mkubwa wa Azimio la Umoja One mnamo Machi 20, 2023?

Jumatatu tutakuwa na maandamano ambayo tuliitisha Februari 22
Tunawahakikishia Wakenya kuwa maandamano yatakuwa ya amani na ni ya kupigania maslahi yao. Waliambiwa baada ya siku 100 bei ya vyakula ingerudi chini.
Katiba inaruhusu kuandamana kwa amani. Hatutajihami, hatutaumiza mtu.
Tulieleza Kenya Kwanza kwamba kulikuwa na mambo matatu tuliyotaka yashughulikiwe. Haya ni; kupanda kwa gharama ya maisha, kusimamisha uteuzi wa makamishina wa IEBC na pia kufunguliwa mitambo yenye matokeo ya Urais kwenye uchaguzi mkuu uliopita. hadi leo hawajayashughulikia.

Hivi majuzi tuliwaona polisi wakiweka vizuizi barabara za kuelekea Ikulu ya Nairobi. Kuna mpango wa kuelekea Ikulu?

Ikulu ni Nyumba ya wananchi. Wafanyabiashara wa Nyamakima hivi majuzi walijitokeza kwa wingi na kuandaa maandamano hadi afisi ya Naibu Rais kisha wakawasilisha malalamishi yao. Wale wa Kisumu waliwasilisha malalamishi yao kwa Kamishina wa Kaunti. Iwapo, Wakenya wangetaka kuelekea Ikulu mnamo Jumatatu kuwasilisha malalamishi yao kwa Rais William Ruto, basi wapo huru kufanya hivyo.
Kifungu cha 37 cha katiba kinampa kila Mkenya haki ya kuandamana. Kwa hivyo, hawahitaji ruhusa ya Ruto. Polisi wanastahili kuwasindikiza wakiamua kuelekea Ikulu, wawakaribishe na waambie Rais watu wako wapo langoni. Kwa hivyo wacheni watu waamue.

Ulidai kuwa huwa mnapokea vitisho. Ni aina gani na kutoka kwa nani?

Walinzi wetu wote waliondolewa na tumepokea kila aina ya vitisho japo tumejiandaa.

Baadhi yetu wanalengwa na kusingiziwa mashtaka kama aliyekuwa waziri Dkt Fred Matiang’i. Hata hivyo, hatutatishwa ili tulegeze kamba.

Miaka ya nyuma, viongozi waliohudumia nchi hii walikuwa wakiachiwa walinzi wachache hata wakistaafu.

Bado huwa mnakutana kama mawaziri waliohudumu chini ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta?

Ndio sisi ni marafiki na huwa tunakutana kunywa chai. Binafsi mimi ni wakili ambaye amehudumu kwa zaidi ya miaka 20 na sasa nafanya kazi ya uwakili. Pia mimi ni mwanafunzi wa Shahada ya Uzamifu. Kwa sasa mimi si waziri nina muda mwingi wa kuwajibikia majukumu yangu kibinafsi.

Unahisi Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta alisalitiwa na wandani wake katika jitihada zake za kuhakikisha Raila Odinga anamrithi?

Hapana. Uhuru hakuwa akiwania Urais na hakusalitiwa na yeyote. Kuna wale ambao wanamwandama sasa na familia yake, na si vizuri.

Ukimwaangalia Jomo Kenyatta, alichukua mamlaka kisha akaenda Nakuru na kutangaza kuwa aliwasamehe Wakoloni waliomzuilia Kapenguria, wakamsingizia mashtaka na kumfunga kwa miaka tisa.
Moi alipoondoka na Rais Mwai Kibaki kuchukua hatamu, hakumfuatilia mtangulizi wake japo Moi hakumuunga mkono.

Uhuru naye hakuandama Kibaki kwa sababu Kibaki naye hakumuunga mkono

Kwa nini Ruto anafuatilia familia ya Uhuru na Moi?

Tukimaliza, una kauli gani kuhusu kesho?

Mwanzo nawarai polisi wawaruhusu Wakenya waandae maandamano Nairobi. Wasikubali watumiwe kukiuka haki za raia.
Wakumbuke kwamba ICC bado ipo na aliyekuwa Inspekta Jenerali wa Polisi alishtakiwa kwa sababu ya mauaji.

  • Tags

You can share this post!

Azimio yaonya polisi kuhusu maandamano

BAHARI YA MAPENZI: Tabia za wazazi hufuata watoto wao hata...

T L