• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
Hamtaniweza, Ruto awaambia mahasidi

Hamtaniweza, Ruto awaambia mahasidi

ERIC WAINAINA na ALEX NJERU

NAIBU Rais William Ruto amesema anajitayarisha kukabiliana na viongozi wanaomlenga kwa propaganda kupitia vyombo vya habari, katika harakati zake za kuwania urais mwaka wa 2022.

Bw Ruto ambaye alikuwa akiongea katika hafla ya kuchangisha pesa katika Shule ya Sekondari ya St Joseph’s Githunguri, Kaunti ya Kiambu Ijumaa, alisema anajua kuhusu makundi ambayo yameanzisha juhudi hizo za kueneza propaganda ili kuchafua sifa ya serikali.

Alieleza kuwa hatishwi na juhudi hizo ambazo alisema zinaendeshwa na watu ambao hakuwataja, akisema rekodi ya serikali ya Jubilee inaonekana dhahiri na kwamba yuko tayari kukabiliana na wanaohusika nazo kwa msingi wa ufanisi wa serikali.

“Kuna jaribio la kuhujumu rekodi ya Jubilee, lakini ukweli huwa haufichiki, hauwezi kufuta rekodi ya serikali ya Jubilee kwa kuwa ni ya kweli. Kwa hivyo, wale wanaoendesha propaganda, wacha waendelee lakini tutakutana nao siku ya kiama (uchaguzi wa 2022) na wapigakura wataamua ni nani mchapa kazi na nani mwenye propaganda,” alisema.

Naibu huyo alieleza kuwa anafahamu vyema kinachoendelea hasa kuhusiana na siasa, na kwamba kuna makundi ambayo yamejipanga kueneza uongo kupitia kwa vyombo vya habari kwa lengo la kuwagawanya Wakenya, lakini akasema vitendo vyao havitamshtua.

Bw Ruto alikuwa ameandamana na viongozi wa eneo la Kati ambao walisema watatimiza ahadi yao ya kumuunga mkono.

Viongozi hao walijumuisha Seneta wa Kiambu Kimani Wamatangi, Naibu Gavana James Nyoro, wabunge Moses Kuria (Gatundu Kusini), Kimani Ichung’wa (Kikuyu), Kago wa Lydia (Githunguri), N’gan’ga Kin’gara (Ruiru), Jonah Mburu (Lari), Jude Njomo (Kiambu Mjini), Rigathi Gachagua (Mathira), Mwakilishi Mwanamke Wambui Ngirichi (Kirinyaga), Faith Gitau (Nyandarua) na Faith Mukami (Nyeri)

Hata hivyo, akiendelea kujitayarisha, wanasiasa kutoka eneo la kaskazini mwa Mlima Kenya wamesema kwamba watamuunga mkono Bw Ruto tu iwapo aatamchagua Senata wa Tharaka -Nithi, Prof Kithure Kindiki, kama naibu wake.

Wakizungumza wakati wa sherehe za ufunguzi wa ofisi mpya ya gavana wa kaunti hyio katika mji wa Kathwana, viongozi hao walisema wanahitaji kuketi na Bw Ruto ili kuhakikisha kwamba wamesikilizana.

Wakiongozwa na Gavana Muthomi Njuki, Seneta wa Meru Mithika Linturi, wabunge Patrick Munene (Chuka /Igambangombe), Kareke Mbiuki (Maara), Gichunge Kabeabea (Tigania Kaskazini) na Moses Kirema (Imenti ya Kati) walisema ni wakati wa eneo hilo kupata kiti cha unaibu rais.

Bw Mbiuki alisema kuwa Prof Kindiki ndiye mwanasiasa mtajika kutoka eneo hilo na ndiye wanayemtarajia awe naibu rais.

“Lazima tuongee kwa kauli moja ili tutoe naibu rais mwaka 2022 na huyo si mwingine bali Prof Kindiki ambaye wamefanya kazi na Bw Ruto kwa wakati mrefu, ” alisema Bw Mbiuki.

Bw Munene alisema kuwa viongozi wa eneo hilo wako tayari kufanya kazi na Bw Ruto na wamejitolea kuwa wanachama wa ‘Team Tangatanga ‘.

You can share this post!

Ongwae anaswa kuhusu mbolea feki, achunguzwa kwa sukari ya...

Uhuru ataka IFMIS iwekwe kaunti zote

adminleo