• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 8:22 PM
Joho, Ruto waua ndoto ya chama cha Wapwani

Joho, Ruto waua ndoto ya chama cha Wapwani

Na CHARLES LWANGA

MATUMAINI ya kuundwa kwa chama cha Pwani yanaendelea kudidimia kwa mara nyingine, baada ya wabunge wandani wa Naibu Rais William Ruto na Gavana wa Mombasa Hassan Joho kuanza kujiondoa kwenye mchakato wa kukumbatia wazo hilo.

Viongozi hao sasa wameanza kutelekeza wazo hilo hasa baada ya Bw Joho ambaye ni Naibu Kiongozi wa ODM, kuwasilisha karatasi zake kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho.

Kwa upande mwingine, wabunge wandani wa Dkt Ruto nao wameasi wazo hilo baada ya Naibu Rais kukumbatia chama kipya cha UDA kutokana na misukosuko inayoendelea ndani ya Jubilee.

Wakati Dkt Ruto alipotembelea Pwani mnamo Februari mwaka huu, aliwataka viongozi wa Tangatanga katika kaunti za Kilifi, Mombasa na Kwale wajiondoe katika kuunda chama cha Pwani na badala yake wajiunge naye katika kunadi vuguvugu la Hasla.

Nalo jaribio la wabunge wa Tangatanga Aisha Jumwa (Malindi) na mwenzake wa Kilifi Kaskazini Owen Baya kufufua chama cha Kadu Asili ambacho kina mizizi yake Pwani liligonga mwamba baada ya kinara wake Gerald Thoya kukataa kuwapokea chamani.

Wabunge wengine wa Tangatanga kutoka Pwani ni Mohammed Ali (Nyali) Khatib Mwashetani (Lungalunga), Sharif Ali (Lamu Mashariki), Jones Mlolwe (Voi), Paul Katana (Kaloleni), Ali Wario (Bura), Benjamin Tayari (Kinango) na aliyekuwa Seneta wa Mombasa Hassan Omar.

Mnamo Jumamosi iliyopita wakati wa mazishi ya Mzee wa Kaya Kahindi Ngowa, Gavana wa Kilifi Amason Kingi ambaye amekuwa akipigania juhudi za kuundwa kwa chama cha Pwani, aliwalaumu wabunge kwa kumtoroka na kukumbatia vyama vingine kuelekea uchaguzi wa 2022.

“Kuna uwezekano kwamba eneo hili bado litashikwa mateka na vyama kutoka nje kwenye uchaguzi wa 2022. Lazima tufikirie mustakabali wetu,” akasema Bw KingiBaadhi ya wabunge kutoka ODM ambao wamejitenga na wazo la kubuniwa kwa chama hicho ni Teddy Mwambire wa Ganze, Ken Chonga (Kilifi Kusini) Seneta wa Kilifi Steward Madzayo na mbunge Mwakilishi wa Kilifi Getrude Mbeya.

Hata hivyo, Bw Mwambire ambaye ni Katibu Mkuu wa kundi la wabunge wa Pwani, alimpuuzilia mbali Bw Kingi akisema kuwa bado hajajibu maswali waliyoibua kuhusu kuundwa kwa chama hicho.Mbunge huyo alikariri kwamba hawawezi kufuata Bw Kingi kisha mwisho wapoteze umaarufu na wapinzani wao waunge na vyama vinavyodhaniwa kuwa ni vya nje kisha kuwabwaga uchaguzini.

“Ni kweli kwamba tumeandaa mikutano mingi na Gavana Kingi kuhusu hili suala la umoja wa Pwani na kuna masuala ya ndani tuliyoyaibua ambayo majibu yake hatujayapata hadi leo,” akasema Bw Mwambire.

Gavana Kingi naye ameshikilia kwamba ataunganisha vyama vidogo vya Pwani akilenga kuwania urais 2022.

You can share this post!

Wakazi walala msituni wakihofu kukamatwa

BBI: Kibarua kwa wabunge kushawishi wafuasi