Na GEORGE MUNENE
Kiongozi wa chama The Service Party, Mwangi Kiunjuri, amepigwa jeki baada ya wawaniaji 20 wa kiti cha udiwani kutoka kaunti ya Kirinyaga kutangaza kuwa watatafuta tiketi ya chama chake kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.
Walitangaza hayo Jumamosi jioni katika eneo la Kianyaga eneobunge la Gichugu wakati wa mkutano wa kuweka mikakati uliosimamiwa na aliyekuwa gavana wa Kirinyaga Joseph Ndathi.Wawaniaji hao walitaja chama cha Bw Kiunjuri kama kilicho na uwazi zaidi eneo la Mlima Kenya na ndio sababu walijiunga nacho.
Walisema wana imani kwamba watashinda uchaguzi kwa kura nyingi katika wadi zote 20 katika kaunti hiyo.“Kando na kuwa na uwazi, TSP kinaendelea kupata umaarufu kwa kiwango kikubwa na ndicho chama chaguo letu,” alisema Idah Murugi anayewania kiti cha udiwani wadi ya Kiini.
Bw Ndathi ambaye pia anagombea tena kiti cha ugavana kwa tiketi ya chama hicho alisema kwamba wawaniaji hao walifanya uamuzi wa busara.“Wamekumbatia chama chetu na sasa tunashughulika na uchaguzi wa 2022.
Wako tayari kutoa huduma bora kwa wakazi wakishinda uchaguzi,” alisema Bw Ndathi.Alisema kwamba chama cha TSP kimeimarika na akasisitiza kuwa chama cha Jubilee kimekosa umaarufu katika kaunti hiyo na eneo la Mlima Kenya.