• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 3:55 PM
Matokeo ya uchaguzi mdogo Kwale yalivyowapa maadui wa Joho sauti

Matokeo ya uchaguzi mdogo Kwale yalivyowapa maadui wa Joho sauti

Na MOHAMED AHMED

SIASA za uchaguzi mdogo wa Msambweni, Kwale uliofanyika mwezi uliopita, zilikuwa zimechukuliwa kama kipimo cha umaarufu na ufuasi miongoni mwa viongozi wa Pwani.

Kati ya viongozi hao ni pamoja na Gavana Hassan Joho na baadhi ya wabunge ambao zamani walikuwa maswahiba wa Bw Joho lakini baadaye wakamtoroka.

Wabunge hao wanaongozwa na Bi Aisha Jumwa (Malindi), Owen Baya (Kilifi Kaskazini), Mohammed Ali (Nyali) na Khatib Mwashetani wa Lunga Lunga.

Wabunge hao walikuwa wameshikana pia na kusukumwa na aliyekuwa seneta wa Mombasa, Bw Hassan Omar ambaye ni mpinzani mkubwa wa Bw Joho.

Katika uchaguzi huo, wapinzani hao walikuwa wanamuunga mkono Feisal Bader ambaye alinyakua kiti hicho dhidi ya Bw Omar Boga ambaye alikuwa anaungwa mkono na Bw Joho.

Kuanzia kumalizika kwa uchaguzi huo, moto wa kisiasa ulianza rasmi kati ya Bw Joho na viongozi hao wenzake wa Pwani. Mzozo huo wa kisiasa baina ya pande hizo mbili pia umelenga kumuondolea Bw Joho sifa za kuwa kiongozi ama “Sultan” wa Pwani kama anavyojiita.

Sasa, wabunge hao wamezamia kwa nguvu mpya, kuendeleza ‘injili’ yao ya kutaka kuwepo kwa chama cha Pwani huku baadhi yao wakimpendekeza Gavana Salim Mvurya wa Kwale kuwa ndiye anayestahili kuwa kiongozi wa Pwani.

“Sisi hatukuogopi. Wewe kama unataka siasa za kujipiga kifua na majivuno basi tunakwambia tuko tayari. Tutapambana na wewe. Kama ulisema huu ndio mwaka utakaoongoza Pwani basi sisi tuko tayari kupambana,” akasema Bi Jumwa wiki jana kufuatia kauli ya Gavana Joho kuwa chama cha ODM kitaanza rasmi kampeni zake mwaka huu.Aidha, wabunge hao wakiongozwa na Bw Baya walisema nembo na rangi za chama wanachotaka kusajili ziko tayari.

Chama hicho kipya, wabunge hao walisema, kinalenga kuendeleza umoja wa Pwani na kujitoa kwenye utawala wa ODM ambapo Bw Joho ndiye naibu kiongozi.

Chama hicho kulingana nao pia kitaungana na vuguvugu la Hustler Nation ambalo linaongozwa na Naibu Rais William Ruto.Wabunge hao walitoa matamshi hayo yote baada ya Bw Joho kutoa taarifa ya akiikashifu mipango yao ya kuunda chama kipya cha Pwani akisema kuwa tayari kuna vyama vya kutosha Pwani.

Badala yake, Bw Joho alidai kuwa viongozi hao wanapanga mipango hiyo ili kumridhisha Dkt Ruto ambaye ndiye kiongozi wao wa mipango hiyo.Mnamo Alhamisi alipozuru Kaunti ya Tana River, Bw Joho kwa mara nyingine aliwafokea wabunge hao na kusema kuwa umoja huo wa Pwani haufai kuelemea kwa kiongozi ambaye wanamtaka wao.

“Msiambiwe tu kushikana kwa sababu ya mtu fulani. Kama ni kushikana, tushikane kwa sababu yetu wenyewe. Mimi nataka kubadilisha hayo mawazo ya kufuata watu wengine. Safari hii sisi tusikubali kuwa wafuasi, ni lazima sisi pia tufuatwe,” akasema Bw Joho.

Alisema kuwa kusimama kwa Pwani na Bw Raila Odinga ni kwa matarajio kuwa ataunga ukanda huo siku za usoni. Bw Joho alisema ukanda wa Pwani unapaswa kulenga kuwa na kiongozi atakayewakilisha eneo hilo katika mjadala wa kitaifa na si kuendelea kuwakilishwa kila mwaka.

“Sisi tutafanya mashauriano na watu wetu.  Hatuwezi kuendelea kufuata kila siku. Tunataka kuwa tunakaa kwenye meza na kuwa na sauti na si kila siku sisi tuwe ndio ‘menu’. Haiwezi kuwa kila hesabu zikipigwa sisi hatumo. Sisi pia tuna uwezo,” akasema Bw Joho.

Kulingana na mchanganuzi wa siasa za Pwani, Prof Hassan Mwakimako viongozi hao wote wamekuwa na tabia ya ubinafsi na kwa muda sasa wanaangalia maslahi yao kuliko yale ya Pwani.

Katika mahojiano, Prof Mwakimako alisema kuwa umoja wa Pwani utasimama iwapo wanasiasa watakuwa na nia safi na wakazi na si kupitia vyama.

“Sioni kama wanasiasa hawa wana nia ya ukweli kuhusiana na umoja wa Pwani. Kama ni umoja si lazima pawepo chama kipya ama tuendelee kukaa kwenye vyama vinavyoongozwa na wengine. Nia ikiwa safi basi hapo ndipo watakapofaulu,” akasema.

Ukiwa umesalia mwaka mmoja hadi kufikia uchaguzi mkuu ujao, itaangaliwa ni vipi ukanda huo utakavyoenda kuhusiana na siasa za 2022 kwani kwa muda eneo hilo limekuwa likiongozwa na wanasiasa wakuu kwa sababu ya mgawanyiko na kutoshikana kwa viongozi kama ilivyo sasa.

Viongozi hao wakuu wameendelea kunufaika na kukosekana kwa umoja wa Pwani ambayo huajawa na kiongozi wa kuiendesha na kuwa na sauti moja kama jamii.

You can share this post!

Uchaguzi mdogo wa useneta Machakos mtihani kwa umaarufu wa...

Mawimbi ya BBI yanavyoyumbisha kundi la Kieleweke