• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 10:50 AM
Mkakati wangu ni wa kuleta maendeleo na amani – Ruto

Mkakati wangu ni wa kuleta maendeleo na amani – Ruto

Na CHARLES WASONGA

NAIBU Rais William Ruto amesisitiza ataendelea kutekeleza ajenda za maendeleo nchini licha ya shutuma anazoelekezewa na baadhi ya maafisa wa serikali.

Akiongea Jumanne alipopokea viongozi wa mashinani kutoka eneobunge la Gatanga katika makazi yake rasmi ya Karen, Nairobi, Dkt Ruto pia alisema ataendelea na kampeni yake ya urais huku akipalilia umoja nchini.

“Nitaendelea kutekeleza miradi ambayo tulianzisha na Rais Uhuru Kenyatta huku tukiwaunganisha Wakenya,” akasema.

Dkt Ruto aliongeza tayari amewaleta pamoja zaidi ya wabunge 150 ambao watasaidia katika utekelezaji wa ahadi ambazo serikali ya Jubilee iliwapa Wakenya.

“Hatutavunjika moyo. Na hatutarudi nyuma,” Dkt Ruto akasisitiza.

Miongoni mwa wabunge waliohudhuria mkutano huo ni pamoja na Rigathi Gachagua (Mathira), Kimani Ichungwa (Kikuyu), George Theuri (Embakasi Magharibi), Isaac Mwaura (Seneta Maalum aliyepokonywa wadhifa wake) na Bw Edward Muriu anayewania kiti hicho cha ubunge cha Gatanga 2022.

Dkt Ruto alitoa kauli hiyo siku moja baada ya Katibu Mkuu wa Jubilee Raphael Tuju na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Amos Kimunya kumwonya vikali.

Wakihutubu katika makao makuu ya chama cha Jubilee mtaani Pangani, Nairobi, wawili hao walioandamana na wabunge wengine wa Jubilee walimtaka Dkt Ruto kuwakanya wandani wake dhidi ya kuikosea heshima familia ya Rais Uhuru Kenyatta.

Aidha, walimtaka kujiuzulu kutoka serikalini badala ya kuendelea kuihujumu na kupinga misimamo na sera zake ilhali yeye ni mshirika ndani ya serikali.

You can share this post!

Malumbano makali kati ya mawakili na DPP kuhusu kesi ya...

Uefa yapinga pendekezo la fainali za Kombe la Dunia...