NA FARHIYA HUSSEIN
NAIBU Gavana wa Mombasa, Dkt William Kingi, amedai kuhangaishwa na maafisa wa usalama wa kaunti hiyo.
Dkt Kingi ambaye ni mwaniaji ugavana Mombasa kupitia Chama cha Pamoja African Alliance (PAA), amedai kuwa maafisa walienda nyumbani kwake kuchukua gari lake rasmi la kazi bila kumwarifu.
“Ni haki yangu kuwa na magari hayo kwa sababu bado nawakilisha afisi ya Naibu Gavana wa Mombasa. Hakuna aliyeniarifu kuwa watachukua magari rasmi. Walikuja nyumbani kwangu wakati ambapo familia yangu ilikuwepo, hiyo haifai,” alisema Dkt Kingi.
Juhudi zetu kuthibitisha madai hayo kwa Serikali ya Kaunti ya Mombasa hazikufua dafu, kwani maafisa waliotafutwa hawakujibu simu.
Dkt Kingi alisema kuwa alilazimika kupeana gari moja kati ya mawili aliyokuwa amepewa na kaunti.
“Hii si mali ya mtu. Bado nahudumu katika afisi hiyo na nitawakabidhi nitakapomaliza muda wangu,” akasema.
Dkt Kingi amekuwa naibu wa Gavana Hassan Joho tangu uchaguzi wa 2017 ulipofanywa.