NA CECIL ODONGO
KINARA wa Azimio la Umoja-One Kenaya, Bw Raila Odinga haonekani kulegeza kamba katika maasi yake dhidi ya serikali licha ya juhudi tele zinazofanywa kumpatanisha na mrengo wa serikali.
Bw Odinga jana Alhamisi aliongoza maandamano ya tatu dhidi ya serikali ambapo makundi ya vijana yalipambana na maafisa wa usalama katika mitaa mbalimbali jijini Nairobi na miji mingine nchini.
Jijini Nairobi, makundi ya vijana yaliokuwa kwenye msafara wa Bw Odinga, yalipambana na polisi katika mitaa ya Imara Daima, Mukuru, Pipeline na Donholm katika barabara ya Outering.
Hata baada ya Bw Odinga kubadilisha njia na kurejea katika barabara ya Ngong baada ya jitihada zake za kuingia katikati mwa jiji kupitia barabara ya Jogoo kugonga mwamba, makundi ya vijana kutoka maeneo ya Eastlands yalipambana na maafisa wa polisi hadi jioni.
Akihutubia umati mkubwa Mukuru, Bw Odinga alishikilia kuwa hata iwapo serikali itawamwaga polisi kila Jumatatu na Alhamisi, hatachoka hadi matakwa yake kuhusu kupanda kwa gharama ya maisha na utata kuhusu uchaguzi mkuu uliopita yatakapotatuliwa.
“Ruto apende asipende mabadiliko yatakuja. Hata akiweka askari wangapi, raia watapita. Tunaleta ukombozi na Wakenya wameonyesha dhahiri kwamba wanataka ukombozi. Pia mitambo ya IEBC lazima ifunguliwe kwa sababu ndiyo iliyo na ukweli kuhusu matokeo ya uchaguzi,” akasema Bw Odinga.
“Ruto anajua kuwa hakushinda uchaguzi mkuu uliopita. Hatutachoka kudai haki yetu hata akiendelea na ukatili wake dhidi yetu,” akaongeza huku akishangiliwa na vijana waliokuwa wakiimba Ruto Must Go (lazima lazima aende).
Msimamo mkali wa Bw Raila dhidi ya utawala wa Kenya Kwanza unaonekana kuendelea kuwa na mashiko kila siku hata baada ya kukutana wa wajumbe kutoka Amerika wakiongozwa na Seneta wa Jimbo la Delaware, Chris Coons Jumatano.
Duru ziliarifu kuwa Bw Coon ambaye pia alikutana na Naibu Rais Rigathi Gachagua alimtaka Bw Odinga asitishe maandamano anayoongoza ila kiongozi huyo wa ODM akakataa akisema shughuli hiyo ilikuwa ishapangwa. Kwenye ukurasa wake wa Twitter, kiongozi huyo alisema walishauriana na seneta huyo kuhusu matukio ya kisiasa nchini.
“Tulishauriana na ujumbe kutoka Marekani ukiongozwa na Seneta Chris Coons. Tulijadiliana kuhusu umuhimu wa kuzingatia Katiba na sheria kuhusu masuala yote,” akaandika Bw Odinga.
Jumatano hiyo, Bw Odinga alikutana pia na Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki (KCCB) ambao walimrai akomeshe maandamano ya jana ili kupisha mashauriano. Bw Raila aliwaahidi maaskofu hao, walioongzwa na Askofu wa Jimbo la Nairobi Phillip Anyolo, kuwa mlango bado u wazi kwa majadiliano ili kurejesha utulivu japo akasisitiza maandamano yataendelea.
Kutokana na mikutano hiyo miwili inakuwa wazi kuwa mara hii kinara huyo wa ODM ameshikilia maamuzi yake kwamba masuala anayoyapigania lazima yashughulikiwe na utawala wa Kenya Kwanza.
Bw Odinga pia amekuwa akipuuza onyo kutoka kwa Inspekta Jenerali wa Polisi, Japhet Koome na Waziri wa Masuala ya Ndani, Prof Kithure Kindiki kuhusu uhalali wa maandamano anayoendeleza.
Prof Kindiki, Jumatano usiku, alituma masharti mapya ya kuandaa maandamano akiagiza Bw Koome kuyatekeleza kabisa ili kuzuia uharibifu wa mali ya raia na watu binafsi.
Hapo jana Bw Odinga, Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka na Waziri wa zamani wa Ulinzi, Eugene Wamalwa walikaidi agizo lake kwamba wasivae magwanda yanayohusishwa na vuguvugu la Movement for Defence and Democracy (MDD) kwa sababu yanafanana na sare ya polisi.