• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 10:55 AM
Raila asisitiza Azimio itakuwa na mwaniaji mmoja kila kiti

Raila asisitiza Azimio itakuwa na mwaniaji mmoja kila kiti

NA JAMES MURIMI

MWANIAJI wa urais wa Azimio la Umoja One Kenya, Raila Odinga amesisitiza kuwa muungano huo utasimamisha mwaniaji mmoja tu kwa kila kiti.

Hii inamaanisha kwamba katika eneo ambapo kuna wawaniaji wawili wanaotumia moja ya vyama 26 vilivyo ndani ya Azimio, mmoja atapokonywa tiketi.

Katika baadhi ya maeneo kuna wawaniaji kutoka vyama tofauti vilivyo ndani ya muungano wa Azimio.

Vilevile, chama cha ODM hakitaruhusiwa kusimamisha wawaniaji katika eneo ambapo Jubilee ina uungwaji mkono mkubwa.

“Tuna vyama 26 ndani ya muungano wa Azimio. Lengo letu kuu ni kuhakikisha kuwa wawaniaji wetu wanashinda viti. Kwa mfano, ODM haijawasilisha wawaniaji katika eneo la Mlima Kenya.

“Kwa upande mwingine, Jubilee haina wawaniaji katika maeneo ya Pwani, Nyanza na Magharibi,” akasema Bw Odinga.

Akizungumza mjini Nanyuki, Kaunti ya Laikipia, Jumatatu ambapo alikutana na wawaniaji wa vyama vilivyo katika muungano wa Azimio, Bw Odinga alisema wataalamu wake wanaendelea kuandaa manifesto inayotoa mwongozo kuhusu jinsi serikali yake itapambana na ufisadi na kuinua uchumi.

“Manifesto hiyo itachapishwa na kuzinduliwa rasmi wiki ijayo. Manifesto hiyo ndiyo itatumiwa katika kampeni zote za Azimio.

“Hatukutaka kuzindua mapema manifesto yetu kwani wapinzani wetu wataiba baadhi ya ajenda zetu,” akasema Bw Odinga.

  • Tags

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Rais na naibu wake wamemkosea heshima Mzee...

Vipusa wafuzu tenisi ya Afrika

T L