NA BENSON MATHEKA
KIONGOZI wa muungano wa Azimio La Umoja-One Kenya Raila Odinga ametangaza masharti na mwelekeo mpya kufuatia ufichuzi kwamba huenda alipokonywa ushindi kwenye uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022.
Akisema ataendelea kutoa siri zaidi kuhusu yaliyofanyika katika uchaguzi wa urais, Bw Odinga alisema kufuatia ufichuzi huo na habari za siri wanazoendelea kupokea, na kutokana na uchunguzi wao, Azimio haitamtambua William Ruto kama rais wa tano wa Kenya na serikali yake ya Kenya Kwanza.
Ufichuzi huo unaodaiwa kutolewa na mfanyakazi wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), unaonyesha kuwa Bw Odinga alishinda uchaguzi huo kwa kura 8,170,353 ikiwa ni asilimia 57.3 dhidi ya Dkt William Ruto aliyepata kura 5,915,973 au asilimia 41.66 ya kura za urais na sio kura 7,176,141 (asilimia 50.49 ) za Dkt Ruto dhidi ya 6,942,930 (asilimia 48.5) za Bw Odinga alivyotangaza aliyekuwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Akisema Azimio imepata matokeo halisi yakiwemo ya wabunge walioibiwa kura, Bw Odinga aliapa kuendelea na mikutano aliyopanga mwaka 2022 kujadiliana na wafuasi wake na kuwapa mwelekeo zaidi.
“Mambo bado, nitaendelea kutoboa zaidi,” kiongozi huyo wa chama ODM aliambia wafuasi wake na kutangaza mkutano mkubwa katika uwanja wa Jacarada, Nairobi, Jumapili ijayo kuanika maovu zaidi aliyodai yalitekelezwa na aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC, Wafula Chebukati.
Aliitaka serikali ya Kenya Kwanza kujiuzulu uongozini akisema kutokana na ripoti walizo nazo kutoka kwa wafichuzi na kutokana na uchunguzi wao tangu mwaka 2022, wapigakura hawakuipatia mamlaka iwaongoze.
“Sisi kama Azimio tunakataa matokeo yote ya uchaguzi wa 2022. Hatuwezi na hatutatambua utawala wa Kenya Kwanza na tunasema serikali yao sio halali,” alisema.
Akidai kwamba Azimio ilishinda urais kwa zaidi ya kura 2 milioni, Bw Odinga aliongeza: “Hatumtambui William Ruto kama rais wa Kenya na vilevile hatutambui maafisa wowote walio ofisini naye.”
Bw Odinga alisema yuko tayari kuongoza Wakenya kusafisha mfumo wa uchaguzi nchini akamtaka Rais William Ruto asitishe mchakato wa kuajiri makamishna wapya wa IEBC.
“Tunataka juhudi zote za Ruto za kuunda IEBC peke yake zikomeshwe mara moja ili Wakenya wenyewe waweze kuunda tume hiyo baada ya kujadiliana kwa haki na usawa,” alisema Bw Odinga.
Waziri Mkuu huyo wa zamani aliongeza: “Niko tayari kufa nikipigana kuona haki katika uchaguzi ikitendeka Kenya. Lazima tusafishe mchakato wetu wa uchaguzi, sitishwi na siogopi.”
Akisema kwamba ana maelezo zaidi kuhusu udanganyifu katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022, Bw Odinga alifufua suala la kukaguliwa kwa mfumo uchaguzi na rekodi za IEBC na shirika huru ili kubaini ukweli wa kilichotendeka.
“Tunataka shirika huru kukagua muundomsingi wote na rekodi za uchaguzi mkuu wa 2022 katika IEBC na ripoti kutangaziwa umma. Hili halina mjadala,” alisema na kuashiria mwanzo wa makabiliano mapya na Rais Ruto na serikali yake ya Kenya Kwanza.
Bw Odinga alisema Azimio inakataa kile alichotaja kuwa ahadi hewa za chama cha United Democratic Aliance (UDA) na akahimiza Wakenya kukataa “sera kandamizi zinazofanya maisha kuwa magumu.”
Bw Odinga aliwataka Wakenya kuungana kushinikiza kuondolewa kwa ushuru ambao umefanya huduma na bidhaa muhimu kama unga, maziwa, sukari, vitabu vya shule, mafuta na stima kupanda.
“Kuanzia leo, tunataka kila Mkenya anaponunua stima kuchunguza kwa makini taarifa aone pesa zinazoenda kwa stima hasa, ushuru na ajiulize hadi lini tutaendelea kuishi hivi,” alisema.
Subscribe our newsletter to stay updated