Na BENSON MATHEKA
NAIBU Rais William Ruto amedai kuwa wapinzani wake wanatumia vitisho dhidi ya washirika wake kabla ya uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Dkt Ruto alisema kwamba licha ya vitisho hivyo, amejitolea kubadilisha nchi akichaguliwa kuwa rais wa tano wa Kenya.
“Waache kututisha kutufanya tuogope. Huu ndio mwaka ambao tutajikomboa kutoka kwa minyororo ya ukabila, vitisho na woga,” alisema.
Akizungumza katika mikutano ya kampeni maeneo tofauti ya mashariki ya Nairobi, Dkt Ruto alihakikishia Wakenya kwamba akiingia mamlakani atatekeleza miradi ya mipango ya kurekebisha uchumi wa nchi.
“Tunataka kukomboa nchi yetu kwa kuhakikisha vijana milioni 4 wanapata kazi au kufanya biashara wakimaliza masomo,” alisema.